Wananchi wa Halmashauri ya Arusha, wilaya ya Arumeru, wametakiwa kutoa ushirikiano kwa wadau wanaoshughulika na harakati za kupinga maswala ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, ili kutokomeza vitendo hivyo kwa maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.
Akizungumza katika kikao cha kujadili taarifa za robo ya mwisho kwa mwaka wa fedha 2018/2019, za Kamati ya Mkakati wa Kuzuia na Kutokomeza Ukatili kwa Wanawake na Watoto- 'MTAKUWWA halmashauri ya Arusha, kamati inayohusisha wadau mbalimbali wa kupinga vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto.
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha Dkt.Wilson Mahera, amefafanua kuwa, licha ya juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, bado kuna changamoto ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto inayosababishwa na mila na dasturi za jamii ya kimasai kwa baadhi ya maeneo.
Dkt. Mahera amesema kuwa, Kamati ya MTAKUWWA ina jukumu kubwa la kupambana na kuelimisha jamii kuanzia nfazi ya familia juu ya mila na desturi za jamii, zinazoendeleza unyanyasaji kwa wanawake na watoto kwa kushirikiana na wadau wanaoshughulika na masuala hayo ndani ya halmashauri.
Aidha Mkurugenzi Maheta, amethibitisha kuwepo kwa vitendo vya ukatili katika halmashauri hiyo, na kuitaja kata ya Laroi kuongoza kwa matukio ya ulawiti kwa watoto na ndoa za utotoni, zinazosababisha watoto kuacha masomo jambo ambalo linapingwa na kupigwa vita kwa nguvu zote, na kuwataka wanajamii kushirikiana na Serikali kupambana na ukatili wa wanawake na watoto katika jamii.
“Kata ya Laroi imekuwa na matukio ya mara kwa mara ikiwemo ulawiti, ubakaji na ndoa za utotoni huku watoto wakikatishwa masomo na nimekuwa nikipokea simu nyingi sana za kesi za huko na kuzishughulikia, niwatake wananchi kupambana na vitendo hivyo vya ukatili kwa ni kinyume cha sheria" amesema Dkt. Mahera
Katika taarifa iliyosomwa na Afisa Maendeleo ya Jamii, halmashauri ya Arusha, Angela Mvaa, imeeleza, kwa kipindi cha miezi mitatu cha kuanzia mwezi Aprili mpaka Juni 2019, jumla ya matukio kumi na saba ya ukatili kwa watoto yameripotiwa, yakiwemo matukio ya ubakaji, mimba za utotoni, ajira kwa watoto, pamoja na ulawiti huku kata ya Lorai ikiongoza kwa matukio ya ulawiti.
Amefafanua kuwa, tayari matukio hayo yote yamefikishwa kwenye vyombo vya sheria na yako katika hatua mbalimbali ili kupata haki ya watoto hao, na kuwataka wanajamii kutoa ushirikiano ili mashauri hayo yaweze kufika mwisho na watoto kupata haki zao.
Angela meongeza kuwa, kuna changamoto ya jamii yenyewe kutokutoa ushirikiano wakati wa mashauri ya watoto, na kusababisha kesi kushindwa kupata ushahidi na mwisho kupoteza haki za watoto hao, huku wazazi wa pande zote wakikubaliana kumalizana kimila, jambo ambalo ni hatari sana kwa mtoto aliyeathirika kutokana na kufanyiwa vitendo vya ukatili.
Hata hivyo wadau hao, wameeleza kuwa elimu duni, mila na desturi zilizopitwa na wakati pamoja na ushirikiano mdogo wa jamii katika kupiga vita ukatili, vinachangia kukosekana kwa haki za watoto na wanawake, hata inapotokea matukio hayo kutolewa taarifa, kwenye vyombo vya sheria.
Wameenda mbali zaidi na kufafanua kuwa, bado jamii ya Kimasaai na imekuwa ikiamini na kuenzi mila na desturi kandamizi, zinazosababisha kuendelea kuwepo kwa kwa matukio ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, ikiwemo tohara na ndoa za utotoni, kuwaachisha watoto wa kiume kuhudhuria masomo kipindi cha kutahiriwa na wengine kupelekwa kuchunga ng'ombe.
Hindu Mbwego ni Mkurugenzi wa Shirika la CWCD linaloshughulika na maswala ya kupinga vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto pamoja na kuinua maendeleo ya vijana na wanawake, amesema kuwa, wazazi na jamii wameshindwa kutekeleza wajibu wao, wa kulinda watoto na badala yake wameisukumia Serikali jukumu hilo.
"Wazazi wameshindwa kutambua wajibu wao wa kuwalea watoto wamekuwa wakiiachia serikali kila kitu kitu ambacho sio sahihi mzazi unatakiwa umfatilie mwanao kwa kila kitu na kama serikali inataka ushirikiano wowote utoe kwani utamsaidia mwanao" amesema mama Hindu
Licha ya changamoto hizi halmashauri kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wamekuwa na mkakati wa kupunguza na kuondoa matukio hayo, kwa kuhamasisha na kutoa elimu kwa jamii kwa makundi tofauti tofauti ikiwemo, watoto kwa kuanzisha klabu shuleni, vijana, wazee wa mila, wanawake kwa lengo la kuwa na uelewa wa pamoja wa kubadilisha mitazamo dhidi ya mila zinamkandamiza mwanamke na mtoto.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.