Na. Elinipa Lupembe.
Timu ya wafadhili wa mradi wa maji wa vijiji vitano, kutoka Idara ya Maendeleo ya nchini Uingereza - DFID Tanzania, imetembelea na kukagua hatua za ujenzi na utekelezaji wa mradi huo wa maji, unaotekelezwa na shirika la WaterAid Tanzania kwa kushirikiana wa halmashauri ya Arusha.
Mradi huo wa maji, ambao kwa sasa umefika hatua ya tatu sasa ya ujenzi wa miundombinu ya kusambazia maji, mara baada ya kukamilika hatua ya kwanza ya usanifu yakinifu na ile ya uchimbaji wa visima kwa ajili ya vyanzo vya maji, visima ambavyo vimechimbwa kwenye shamba la kilimo la Ilkiushini, kwenye Kitongoji cha Ekenywa kata ya Olturumet.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua ujenzi wa miundo mbinu ya mradi huo, mtalamu Mshauri wa Miradi ya Maji na Usafi wa Mazingira - DFID Tanzania, Lucas Kwezi, amewataka wakandarasi waliopewa zabuni hizo za ujenzi, kuongeza kasi ya ujenzi na utekelezaji wa mradi huo, ili kuweza kukamilisha kazi hizo, kwa muda uliopangwa, kwa kuwa wananchi wanahitaji maji kwa haraka.
Kwezi ameongeza kuwa, licha ya kuwa mradi huo, umeanza kutekelezwa katika maeneo yote ya mradi, amewasisitiza wakandarasi hao, kuhakikisha wanakwenda na muda ambao upo kwenye mikataba ya zabuni zao, na kusisitiza kuwa kazi hizo zinatakiwa kukamilika mwezi Aprili.
Naye Mhandisi Mkaazi wa Shirika la WaterAid Tanzania, Jailosi Chilewa, amesema kuwa, mpaka sasa utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya mradi huo, umefikia asilimi 15 na unategemea kukamilika mwishoni mwa mwezi April mwaka huu.
Mhandisi Chilewa, ameeleza kuwa, ujenzi huo unatekelezwa kwa kugawa kazi katika sehemu kubwa tatu, ambazo kandarasi hizo zimetolewa kwa makampuni matatu, na kuzitaja kampuni hizo ni pamoja na kampuni ya STS Construction Company Ltd, ambayo kandarasi yao itahusisha ujenzi wa miundombinu ya maji, ikiwemo ujenzi wa matanki ya kuhifadhia na kuchujia maji, usambazaji wa mabomba, nyumba za kusambazia maji pamoja na vituo ishirini vya kuchotea maji, kutoka kwenye chanzo cha maji cha Emurtoto kuelekea Olkokola mpaka Lengijave kwa gharama ya shilingi bilion 4.1.
Ameendelea kueleza kuwa, Kazi ya pili inatekelezwa na Mkandarasi wa kampuni ya Advance Company Ltd na Meero Contractors Ltd, inafanya kandarasi ya kujenga nyumba za kusukuma maji, matanki mawili ya kukusanyia maji, tanki moja la kuhifadhia maji, nyumba ya kuhifadhia mitambo ya kutibu maji, kusamba mabomba kutoka kwenye vyanzo vya maji vya Ilkiushini mpaka kwenye tank la kukusanyia maji la Leomoja kwenda Lengijave kwa gharama ya shilingi bilionj 1.7.
Aidha kazi ya tatu inafanywa na mkandarasi wa kampuni ya ASES Ltd, ambao watajenga matanki 2 ya kuhifadhia maji, watasambaza mabomba umbali wa Kilomita 34 kutoka Lemoja kwenda Ekenywa na Lemoja kwenda tanki la Ngaramtoni na kujenga vituo 46 vya kuchotea maji kwa gharama ya shilingi milioni 937.
Awali mradi huu ulianza mwaka 2017 na ulitarajiwa kamilika mwezi Mei mwaka uliopita wa 2018, hata hivyo mradi huo, ulishindikana kukamilika kutokana na changamoto za kiufundi, zilizosababisha kuongezeka kwa gharama za ujenzi wa miundombinu ya kusambazia maji pamoja na mitambo ya kuchujia maji, iliyolazimu serikali kutafuta tena fedha za kugharamia kiasi hicho cha fedha kilichoongezeka.
Hata hivyo Idara ya Maendeleo Uingereza - DFID, walikubali kuongeza kiasi cha fedha, kutoka shilingi bilioni 4.4 mpaka kufikia shilingi bilioni 9.5, gharama ambazo zitakidhi kukamilisha mradi huo, hivyo wananchi wa vitongoji vya Olmotony, Ekenywa na Seuri na vijiji vya Olkokola na Lengijave wategemee kupata maji safi na salama kabla ya kumalizika mwaka huu wa fedha Julai 2019.
Aidha wito umetolewa kw wananchi wote wanaoishi kwenye maeneo yote, ambayo utekelezaji wa mradi unafanyika, kushirikiana na wakandarasi na watalamu wanaotekeleza mradi huo, pamoja na kulinda vifaa vinavyoletwa na wakandarasi kwa ajili ya kujengea miundombinu hiyo.
PICHA ZA MATUKIO YA ZIARA HIYO.
Tanki la Maji Lemoja ambalo litakusanya maji kutoka tanki la Hazina na Ekenywa na kuyasukuma kwenda tanki la maji Kilimapunda na kusambazwa kwa wakazi wa Olmotony eneo la Ngaramtoni
Ujenzi wa tanki la maji Olkokola uko hatua za awali, tanki ambalo litapokea maji kutoka tanki na Hazina na kuyapeleka tanki la Lengijave.
Mitaro iliyochimbwa kwa ajili ya kusimika mabomba ya kusambazia maji kutoka Lemoja kuelekea Ekenywa, na Lemoja mpaka Ngaramtoni, umbali wa Kilomita 34.
Majengo yanayojengwa kwenye shamba la mbegu Ekenywa.
Jengo la kuhifadhia mitambo ya kuchuja na kutibu maji linalojengwa kwenye shamba la mbegu Ekenywa.
Tanki la kukusanyia maji linalijengwa kwenye shamba la mbegu Ekenywa.
Nyumba ya kuwekea pumpu za kusukumia maji.
Mitambo ya kujengea tanki la Hazina
Baadhi ya mabomba yakiwa kwenye eneo la mradi tayari kwa kutandikwa kwenye mitaro iliyochimbwa.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.