Serikali ya awamu ya tano, inayoongozwa na mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli,imefufua matumaini yaliyotoweka kwa wananchi wa kata ya Oldonyosambu kutokana na adha kubwa ya upatikanaji wa maji pamoja na madini hatari ya Floraidi yanayopatikana kwenye maji wanayoyatumia katika eneo lao.
Matumaini hayo yamerejea, mara baada ya wananchi hao wa Oldonyosambu kusimamisha msafara wa mheshimiwa Rais, katika eneo la madukani, wakati akitokea kwenye ufunguzi wa Kituo cha Forodha (OSBP), kwenye mpaka wa Tanzania na Kenya eneo la Namanga.
Wananchi hao walifanikiwa kumueleza mheshimiwa Rais, tatizo kubwa la maji linalowakabili katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na athari kubwa wanazozipata wananchi hao, wanapotumia maji ya eneo hilo yenye kiasi kikubwa cha madini ya Floraidi, kinachowasababishia matatizo ya kiafya na kisaikolojia huku baadhi ya watoto wakizaliwa na vichwa vikubwa na wengine kupinda miguu.
Mheshimiwa Rais, zaidi ya kuwasikiliza hakusita kuwaahidi kushughulikia tatizo hilo na kuamua kuthibitisha hilo katika hotuba yake, aliyoitoa wakati akiwahutubia wananchi wa Arumeru, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Olmringaringa kata ya Kimnyaki, mara baada ya kuweka jiwe la msingi kwenye visima 20, vitakavyotumika kupeleka maji katika maeneo ya Jiji la Arusha, kupitia mradi mkubwa wa maji wenye kugharimu shilingi bilioni 520.
Katika mkutano huo, Mheshimiwa Rais ameuagiza uongozi wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira 'AUWASA' unaosimamia utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa maji, kuhakisha kuwa wananchi wa Oldonyosambu, nao wanapata maji kupitia mradi huo ili kuwanusuru na madhara wanayoyapata kutokana na matumizi ya maji wanayoyatumia yenye kiasi kikubwa cha madini ya floraidi.
Sambamba na hotuba hiyo, ahadi hiyo ya mheshimiwa Rais iligongewa msumari na Waziri wa Maji na Umwagiliaji Profesa Makame Mbalawa, alipokwenda kuonana na wananchi wa Oldonyosambu, na kushuhudia baadhi ya wananchi waliopinda miguu kutokana na tatizo la Floraidi.
Aidha Waziri Mbalawa alitoa pole kwa wananchi hao na kuwahakikishia kuwa, Oldonyosambu itaingizwa kwenye vijiji nufaika vya mradi mkubwa wa maji, uliowekwa jiwe la msingi na mheshimiwa Rais na kuwanya tatizo la wananchi kuathirika na madini ya Floraidi kufika mwisho.
"Niwape pole sana ndugu zangu mliopata madhara yatokanayo na maji yenye madini ya Floraidi na wanaoldonyosambu kwa ujumla, lakini niwahakikishe kama mheshimiwa Rais alivyoagiza, lazima mpate maji safi na salama kupitia mradi huu wa Jiji la Arusha, haiwezekani watu Jiji la Arusha wapate maji ya kutosha huku ninyi mkiendelea kuteseka" amethibitisha Waziri Mbalawa.
Aidha Waziri Mbalawa amewasisitizia wananchi hao kuwa serikali kwa kushirikiana na AUWSA, wataleta watalamu wapitie vijiji vyote vya Oldonyosambu ili kupata idadi ya magati yanayohitajika pamoja na kumsimamia mkandarasi usiku na mchana ili muweze kupata maji safi na salama kwa haraka na kuongeza kuwa endapo mkandarasi atababaisha tutafukuza na kumpa mwingine huku akisisitiza kuwa, pesa tunazo, nia tunayo, na serikali imajipanga kuwaletea maji safi na salama yasiyo na floride yenye madhara kwa viumbe hai.
Ameongeza kuwa Serikali ya awamu ya tano, imejipanga kuhakikisha ifikapo mwaka 2020 asilimia 85% ya wananchi watapata maji safi na salama huku asilimia 90% ya wananchi wa mijini watakuwa wamepata maji safi na salama.
Hata hivyo Mkuu wa mkoa wa Arusha mheshimiwa Mrisho Gambi, alimuomba Waziri huyo wa Maji, kuchangia mifuko ya saruji ambayo wananchi hao wanahitaji kwa ajili ya ujenzi na umaliziaji wa miundombinu ya shule ya sekondari Oldonyosambu, bila kusita Waziri huyo ameahidi kutoa mifuko 100 ya saruji na kufafanua kuwa saruji hiyo itakabidhiwa kwenye Ofisi ya mkuu wa mkoa wa Arusha na ofisi hiyo itafikisha Oldonyosambu, tayari kwa kuanza kufanyiwa kazi iliyokusudiwa.
Kwa upande wao wananchi wa Oldonyosambu, wameipongeza serikali ya awamu ya tano, na zaidi kumshukuru mheshimiwa Rais kwa kusikiliza ombi lao na kulifanyia maamuzi ndani ya siku moja, na kumuomba mheshimiwa Rais kusimamia ahadi hiyo itekelezeke kwa wakati ili kuweza kuzuia tatizo linalowapata kwa miaka mingi sasa.
Minengera Kiroka mkazi wa Oldonyosambu amemshukuru Rais Magufuli, kwa utendaji kazi wake usiolala, wananchi wa Oldonyosambu, tumempa kero yetu jana, leo tuu, ameshatoa tamko kwa ajili ya utekelezaji na zaidi kumuagiza Waziri wa Maji kuja kutuona, na kustaajabu kuwa hali kama hii haijawahi kutokea tangu kuzaliwa kwake hapo Oldonyosambu.
Naye Mwajuma Mustafa licha ya kushukuru Serikali, amasema kuwa wanaamini tatizo hilo sugu litafikia ukingoni na watu hawatapata ulemavu tena, pamoja na kuwapunguzia wanawake adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji safi na salama.
" Kinamama wanateseka sana kutafuta maji ya kunywa na kupikia, tunatembea Kilomita 20 kupata ndoo moja, wakati mwingine wanawake wanashindwa na kuacha familia kunywa maji yenye Floraidi ambayo madhara yake ni makubwa kama mlivyoshuhudia" amesema Mwajuma
Awali Diwani wa kata ya Oldonyosambu, mheshimiwa Raymond Lairumbe alimuelezea tatizo kubwa wanalolipata wananchi wa Oldonyosambu huku madhara zaidi yakiwapata wakazi wa kijiji cha Lemanda, kijiji ambacho kiko mbali zaidi na eneo ambalo wananchi wa vjiji vingine huenda kuhemea kupata walau maji, kwa ajili ya matumizi ya kunywa na kupikia.
Aidha Diwani huyo alipata fursa ya kuyataja madhara wanayoyapata wananchi kutokana na matumizi ya maji ya eneo hilo yenye kiasi kikubwa cha madini ya Floride, ikiwa ni pamoja na meno kuwa na rangi ya kahawia, watoto kuzakiwa na vichwa vikubwa, watu kupinda miguu na kuwa walemavu huku madhara hayo mpaka sasa kutokuwa na tiba pindi mtu anapoathirika.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.