Na. Elinipa Lupembe.
Kampuni ya Tanzania Big Game Safaris Ltd kupitia mradi wake wa Conservation foundation Tanzania wamejenga na kukabidhi rasmi msaada wa vyumba viwili vya madarasa na ofisi ndogo ya walimu, kwa shule ya msingi Musa kata ya Musa halmashauri ya Arusha, mara baada ya kukamilika kwa ujenzio huo, katika hafla fupi iliyofanyika shuleni hapi mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kampuni hiyo, ilifikia hatua ya kutoa msaada huo wa ujenzi wa vyumba hivyo vya madarasa, ujenzi uliogharimu takribani shilingi milioni 50, kufuatia kuguswa na hali mbaya ya uchakavu wa majengo ya shule hiyo, uchakavu uliotokana na majengo hayo kujengwa miaka zaidi ya 60 iliyopita na kuhofia madhara ambayo yangewapata wanafunzi pindi majengo hayo yangeanguka.
Akizungumza kwa niaba ya mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, baada ya kukabidhiwa na kuzindua vyumba hivyo vya madarasa, mkuu wa Idara ya Mifugo na Uvuvi, Charles Ngilorit, amewashukuru wadau wa kampuni hiyo kwa kuguswa na hali ya uchakavu wa majengo uliokuwepo, sambamba na kuunga mkono juhudi za serikali kwa kutoa elimu bila malipo, sera iliyotoa fursa kwa watoto wengi kujiunga na shule hali iliyosababisha upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa.
" Niwapongeze kwa kuwezesha mazingira bora ya watoto wetu, yanayorahisisha tendo la kujifunza na kufundisha, serikali inahitaji suport yenu wadau na inathamini pale mnapojitolea kwa ajili ya jamii, katika maeneo mnayofanyia kazi" amesema Ngilorit.
Aidha ameyataka makampuni mengine ya kitalii kuiga mfano huo, kusaidia kuwekeza kwenye elimu, kwani serikali inahitaji msaada katika mkakati wake wa kuboresha sekta ya elimu hususani kwenye miundombinu ya shule pamoja na samani.
Meneja wa Kampuni ya Tanzania Big Game Safaris Ltd, Webista Kapaliswa amesema kuwa, lengo la kujenga vyumba hivyo vya madarasa ni kusaidia uwezeshaji wa kutoa elimu katika mazingira rafiki, msukumo uliotokana na hali majengo chakavu ya madarasa, yaliyotishia usala wa watoto.
Amesema kampuni iliguswa na hali halisi iliyokuwepo shuleni hapo na kuamua kufadhili ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa, sambamba na kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano ya elimu bila malipo, ilisababisha ongezeko kubwa la watoto shuleni, na kusababisha uhaba wa vyumba vya madarasa.
Hata hivyo meneja huyo amesema kuwa, kampuni yao inafanya kazi katika hifadhi ya mlima Monduli ulioko karibu na eneo la Musa hivyo, kampuni kulazimika kufanya hisani kwa kurudisha kiasi cha faida kinachopatikana kwa jamii ambayo imezunguka hifadhi na hushiriki kutunza mazingira ya hifadhi hiyo.
Aidha amewataka wananchi kuendelea kushiriki katika utunzaji wa mazingira, na kuacha tabia ya kuingiza mifugo kwenye hifadhi ya mlima, mifugo ambayo husababisha uharibifu mkubwa, uharibifu unaohofiwa kukausha vyanzo vya maji na kusababisha ukame na hatimaye jangwa.
Naye mwalimu mkuu wa shule ya msingi Musa, Elizabeth Mollel amesema awali walikuwa na vyumba vya madarasa vitano ambavyo ni chakavu, na kusababisha upungufu wa vyumba vinne, na kuongeza kuwa Kampuni hiyo imepunguza adha hiyo kwa asilimia 50, na kuwaomba wadau wengine wa elimu kuwasadi kupata vyumba 2 tena vya madarasa ili kuondoa kabisa tatizo hilo shuleni hapo.
Glory Elibariki mwanafunzi wa darasa la sita, ameishukuru kampuni hiyo kwa niaba ya wanafunzi wenzie na kuthibitisha adha kubwa waliyokua wakiipata kutokana na kusomea kwenye madarasa chakavu, yaliyotishia usalama wa maisha yao, na kuahidi kusoma kwa bidii kutokana na kuwa na mazingira bora sasa.
Shule ya Msingi Musa ni moja ya shule kongwe nchini, ilianzishwa mwaka 1954, kwa sasa ina jumla ya wanafunzi 619 wavulana 218 na wasichana 222, huku kukiwa na ongezeko kubwa la uandikishaji wa wanafunzi wa kuanza darasa la awali na la kwanza mwaka huu, jumla ya wanafunzi 179 wameandikishwa, ikiwa wavulana 81 na wasichana 98.
PICHA ZA MATUKIO YA MAKABIDHIANO NA UZINDUZI WA MADARASA HAYO.
Vyumba viwili vya madarasa na ofisi ndogo ya walimu iliyojengwa na kampuni ya Tanzania Big Game Safari Ltd katika shule ya Msingi Musa.
Mkuu wa Idara ya Mifugo Charles Ngilorit akizindua majengo ya vyumba vya madarasa, mara baada ya kukabidhiwa na Kampuni ya Tanzania Big Game Safari Ltd.
Meneja wa Kampuni ya Tanzania Big Game Safari Ltd, Webista Kapaliswa, akizungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Musa mra baada ya kukukabidhi mradi wa vyumba vya madarasa, wakati wa hafla ya makabidiano wa mradi huo.
Wanafunzi wa shule ya msingi Musa, wakiimba shairi la kishukuru Kampunibya Tanzania Big Game Safari Ltd kwa kuwajengea madarasa, wakati wa hafla ya kukabidhiwa na uzinduzi wa vyumba viwili vya madarasa shuleni kwao.
Wanafunzi wa shule ya msingi Musa, wakipiga makofi wakati wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa vyumba viwili vya madarasa shuleni kwao.
Wawakilishi wa Kampuni ya Tanzania Big Game Safari Ltd, wakionesha cheti cha utambuzi, cheti walichokabidhiwa kama asante na halmashauri ya Arusha.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.