Hatimaye watoto wa kijiji cha Losikito kata ya Mwandeti, halmashauri ya Arusha wilayani Arumeru, watakaojiunga na elimu ya sekondari kuanzia sasa, wamepata neema, baada ya wazazi wao kuwaonea huruma na kuamua kuwajengea shule mpya ya sekondari katika kijiji chao, na kuwafanya watoto hao kuacha kutembea umbali mrefu kwenda kusoma vijiji na kata za jirani.
Neema hiyo imekuja mara baada ya wazazi wa watoto hao, kuona kero kubwa wanayoipata watoto wao, ya kutembea umbali wa zaidi ya Kilomita kumi kwenda na kurudi shuleni kila siku, jambo ambalo limewasukuma wazazi hao, kuingiwa na huruma na kuanza ujenzi wa shule ya sekondari katika kijiji cha Losikito ili kuwaondolea watoto wao adha hiyo.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini kwao, wengi wa wnanchi hao wamethibitisha kufikia hatua hiyo baada ya kijiji hicho, kutokuwa na shule ya sekondari jirani na kusababisha watoto wao, wanaojiunga na elimu ya sekondari, kutembea umbali mrefu kwenda kufuata elimu kwenye kijiji na kata za jirani, shule ambazo zote ziko mbali na eneo hilo.
Wamesema kuwa umbali mrefu wanaotembea wanafunzi, umekuwa ni changamoto kubwa hasa kwa watoto wa kike, ambao wanakabiliwa na vikwazo vingi njiani huku baadhi ya watoto wakikata tamaa na kuamua kucha kuendelea na shule na wengine kushindwa kufanya vizuri katika masomo yao.
Kimani Lowasare mjumbe wa serikali ya kijiji cha Losikito, amesema kuwa, watoto wengi wanashindwa kufikia malengo yao kielimu, kutokana na umbali mrefu wanaotembea kwenda na kurudi shuleni kila siku na kusababisha kupoteza kabisa ndoto zao.
Ameongeza kuwa, viongozi wa wananchi na wazazi, tuliona changamoto kubwa inayowakabili watoto wetu ya kushindwa kufikia malengo yao ya kielimu, na kuamua kufunga mikana na kuchangishana fedha ili kupata nguvu ya pamoja, iliyowezesha kujenga majengo haya, lengo likiwa ni kuhakikisha watoto wao, wanapata elimu ya sekondari hapa karibu na si kwenda mbali tena.
" Vijana wetu wanateseka sana wakimaliza darasa la saba, hapa hakuna shule ya sekondari, wanatembea mpaka Mwandet sekondari, inakatisha tamaaa wengi hawafikii malengo yao, ndio maana wananchi wa Losikito, tumeamua kuchangishana na kujenga shule ya sekondari Losikito" amesema Lowasare
Kwa upande wake Lazaro Mollel mwananchi wa Losikito, amesema kuwa umbali mrefu si salama hasa kwa watoto wa kike na umekuwa ukiwathiri wengi wao, kimasomo huku baadhi yao wakifanyiwa matukio ya ukatili njiani na wengine kupata mimba na kuacha shule, jambo ambalo wazazi tumeona tulidhibiti kwa kuwajengea shule jirani.
Naye Diwani wa kata ya Mwandeti, mheshimiwa Boniface Tarakwa, amethibitisha adha waliyokuwa wanaipata watoto wa Losikito, kwa kwenda kusoma vijiji vya jirani na kusema kuwa wananchi wake wameungana na kuamua kuanzisha shule ya sekondari kijiji hapo kwa kuanza kujenga miundombinu ya vyumba vinne vya madarasa, vyoo, nyumba ya walimu pamoja na ofisi za walimu.
Ameongeza kuwa licha ya kuwasaidiwa watoto kutembea umbali mrefu kwenda shuleni lakini ujenzi wa shule ya Losikito itapunguza idadi kubwa ya wanafunzi katika shuele ya kata ya Sekondari Mwandet, shule ambayo inachukua idadi kubwa ya wanafunzi kulinganisha na uwezo wa majengo ya shule hiyo.
"Shule ya sekondari ya Mwandet ina chukua watoto wa kata nzima ya Mwandeti na kata nyingine ndani ya halmasgauri na kufanya kuzidiwa na idadi kubwa ya wanafunzi, hivyo ujenzi wa shule hii mpya utapunguza population inayoielemea sekondari ya Mwandeti" amesema diwani huyo
Naye Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Dkt. Wilson Mahera, licha ya kuwapongeza wananchi wa Losikito kwa juhudi kubwa walizozifanya za kuboresha na kuendeleza sekta ya Elimu, amewathibitishia wananchi hao kuhakikisha usajili wa shule hiyo unafanyika kwa haraka, pamoja na kuleta walimu, vifaa vya kufundishia na kufundishia ili ifikapo Januari 2019 wanafunzi wa kidato cha kwanza wapangiwe shuleni hapo.
Ameongeza kuwa, ujenzi wa shule hii umefanyika wakati muafaka kwa kuwa, kumekuwa na ongezeko la ufaulu kwa wanafunzi wa darasa la saba waliofanya mitihani yao mwaka huu 2018, ufaulu ambao umesababisha halmashauri kuwa na uhaba wa vyumba vya madarsa 109, kwa wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa mwaka ujao wa masomo wa 2019.
"Tayari taratibu zote za usajili zinaendelea, hivyo shule hii itaanza kuchukua wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2019 na kupunguza idadi ya vyumba vya madarasa vinavyohitajika" amefafanua Dkt. Mahera
Hata hivyo, Mwenyekiti wa kijiji cha Losikito, Logorie Masandaguwa, amethibitisha kuwa wananchi wa kijiji cha Losikito, wameridhishwa na uongozi wa serikali ya awamu ya tano, unaoongozwa na Rais Magufuli, uongozi wenye usimamizi imara wa mali ya Umma, unaowapa hamasa ya kujitoa na kuchangia miradi ya maendeleo katika eneo lao, tofauti na hapo awali usimamizi ulikua unalegalega.
"Tunaona namna serikali yetu inajitoa kwa wananchi hadi wa vijijini, hii inawajengea imani wananchi na kuiamini serikali yao, na pia inawapa hamasa hata wananchi kuingia mfukoni kuchangia maendeleo katika kijiji chetu, tofauti na zamani wananchi walikata tamaaa na kuhofia fedha zao kuishia kwenye matumbo ya wajanja wachache" amethibitisha Mwenyekiti huyo.
Awali, wananchi wa kijiji cha Losikito, kupitia miradi ya Jitihada za Jamii (JJ), kwa kuchangishana kiasi cha shilingi 125,00/= kwa kila mwananchi na kufanikiwa kuanza ujenzi wa miundombinu ya shule hiyo, ikiwa ni pamoja na kujenga vyumba vinne vya madarasa na vyoo, ofisi ya walimu, pamoja na nyumba ya walimu yenye uwezo wa kuishi familia tatu ' 3 in 1' vyenye thamani ya shilingi 257.9 huku halmashauri ikiwaongezea nguvu kwa shilingi milioni 6, ujenzi ambao kwa sasa uko katika hatua za mwisho za ukamilishaji.
Hata hivyo, wananchi hao wamefanya ukarabati wa jengo lililokuwa linatumika kama ofisi na halmashauri Kuu ya kijiji, ili liweze kutumika kama jengo la utawala la shule hiyo na tayari wana mkakati wa kuanza kujenga maabara kwa ajili ya masomo ya Sayansi mapema mwezi ujao.
Nyumba ya walimu shule ya Sekondaro Losikito.
Jengo lilikuwa ofisi ya halmashauri kuu ya Kijiji cha Losikito, kwa sasa linatarajiwa kuwa jengo la utawala shule ya sekondari Losikito , likiendelea kufanyiwa ukarabati
Muonekano wa mbele wa Jengo linalotarajiwa kuwa jengo la utawala shule ya sekondari Losikito , baada ya kukamilika kufanyiwa ukarabati.
Baadhi ya vydumba vya madarasa shule ya sekondari Losikito.
Jengo la choo cha wanafunzi, shule ya sekondari Losikito
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.