Na. Elinipa Lupembe.
Maafisa Watendaji wa Kata na Vijiji, halmashauri ya Arusha, wametakiwa kuzingatia mkakati wa Serikali juu ya masuala ya Lishe bora ya wananchi katika maeneo yao, kupitia mkataba wa Lishe waliosaini, lengo likiwa kuondoa hali ya udumavu katika jamii na kuwa na jamii yenye afya bora.
Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhandisi Richard Ruyango, wakati akifungua kikao kazi cha mkatati wa Lishe, kilichojumuisha Maafisa Watendaji wa Kata na Vijiji, halmashauri ya Arusha, chenye lengo la kufanya tathmini ya hali ya lishe kwa miaka mitano iliyopita na kusaini mkataba wa mkakati wa Lishe kwa miaka mitano ijayo, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
Mhandisi Ruyango, amewaagiza watendaji hao, kuwa na mkakati shirikishi, utakaowashirikisha wananchi, Wahudumu wa Afya, wahudumu wa Afya ngazi ya jamii pamoja na wadau wa maendeleo, kutoa elimu ya Lishe kwa jamii, ili kuhakikisha wananchi wote wanapata ufahamu juu ya lishe bora, hususani kwa wajawazito na watoto.
"Ninawagiza watendaji wote, Lishe iwe agenda ya kudumu katika vikao vyenu vyote kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji, kata pamoja na menejimenti kwa kuwashirikisha waheshimiwa Madiwani, lengo likiwa kuondoa udumavu wa mwili na akili kwa wananchi wote maeneo yotu, kupitia tathmini ya miaka mitano iliyopita, tunatakiwa kufanya vizuri zaidi kwa miaka mitano ijayo" amesisitiza Mkuu huyo wa Wilaya.
Aidha Mkuu huyo wa wilaya amewasisitiza Watendaji hao, kuhakikisha kina mama Wajawazito katika maeneo yao wanapata Lishe bora katika siku 1000 za ujauzito, lishe ambayo tafiti zinaonesha ndio inawezesha mtoto aliye tumboni kujenga afya bora ya ubongo na mwili, afya ambayo ndio inategemewa na jamii na Taifa hapo baadaye na kuwasisitiza kutumia vyakula kutoka makundi matano ya vyakula, vyakua ambavyo vinapatikana katika maeneo yote ya Arumeru.
Naye Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, amewataka Maafisa watendaji hao, kuhakikisha wajawazito wote katika maeneo yao wanahudhuria kliniki pindi wanapopata ujauzito, wazazi wote wenye watoto wa umri chini ya miaka mitano kuwapeleka watoto hao kliniki, pamoja na kupiga vita tabia ya kina mama wajawazito kujifungulia nyumbani sambamba na kuweka sheria ndogo za kuwashughulikia wale watakaokiuka.
"Ninawasisitiza Maafisa Watendaji wote wa kata na vijiji kufanya kazi kwa kushirikiana kama timu, ili kuhakikisha wananchi wenu wanakula vyakula kwa kuzingatia makundi yatakayowapa lishe bora, wananchi wakiwa na afya bora nguvu kazi itaongezeka na wananchi wakiwa na nguvu, wataleta maendeleo katika maeneo yetu" ameweka wazi Mkurugenzi Msumi.
Afisa Mtendaji Kata ya Ilboru, Wema Sikoi, amekiri kupata uelewa mkubwa juu ya masuala ya Lishe, na kuahidi kwenda kufanyia kazi maelekezo yaliyotolewa na serikali kulingana na mkataba waliousani, na kuongeza kuwa, wataongeza kasi ya kuhakikisha wajawazito wanahudhuria kiliniki na wenza wao, pamoja na kuwapatia lishe bora katika siku 1000 za ujauzito, siku ambazo zinaonekana kuwa ni msingi wa afya ya binadamu yoyote.
Hata hivyo Afisa Lishe, Halmasahuri ya Arusha, Doto Milembe, ameyataja makundi ya vyakula yanayopaswa kuliwa ili mtu kuwa na lishe bora ni vyakula vya nafaka na mizizi, vyakula vya nyama na mikunde, mbogamboga na matunda pamoja na sukari na asali na kubainisha kuwa vyakula vyote hivyo vinapatika katika maeneo mengi ya halmashauri ya Arusha.
Awali serikali imeandaa mpango wa Lishe wa miaka mitano 2022 -2027, unaotaka kila mwananchi kuwa kupata lishe bora kwa kula mlo wenye makundi matano ya vyakula kuanzia siku 1000 za mama mjazito, mtoto anapozaliwa mpaka miaka mitano na jamii nzima, mkakati unaoelekeza kuwasainisha mikataba Maafisa Watendaji wa Kata ili kusimamia mkakati huo wa Lishe.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍✍
Mkuu wa wilaya ya Arumeru, Mhandisi Richard Ruyango, akizungumza na Maafisa Watendaji wa Kata na Vijiji, halmashuri ya Arusha wakati akifungua Kikao kazi cha tathmini ya Lishe kwa miaka mitano na kuweka mikakati ya miaka mitano ijayo, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano halmashauri ya Arusha.
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, akizungumza na Maafisa Watendaji wa Kata na Vijiji, halmashuri ya Arusha wakati wa Kikao kazi cha tathmini ya Lishe kwa miaka mitano na kuweka mikakati ya miaka mitano ijayo, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano halmashauri ya Arusha.
Afisa Mtendaji Kata ya Kiutu, Twati Sukurieti akiweka saini mkataba wa kisimamia masuala ua Lishe katika kata yake kwa kipindi cha miaka mitano, wakati wa Kikao kazi cha tathmini ya Lishe kwa miaka mitano mikakati ya miaka mitano ijayo, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano halmashauri ya Arusha.
Afisa Lishe halmashauri ya Arusha, Doto Milembe, akitoa tathmini ya hali ya Lishe ya halmashauri ya Arusha katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na mikakati ya miaka mitano ijayo, wakati wa Kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano halmashauri ya Arusha.
Maafisa Watendaji wa kata na Vijiji wakisaini mikataba ya Lishe yenye mikakati ya Lishe katika maeneo yao kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, wakati wa Kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano halmashauri ya Arusha
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.