Na mwandishi wetu
Kampuni ya Itracom Fertilizers Limited Tanzania imeanza utengenezaji wa mbolea ya Ruzuku ya FOMI nchini Tanzania inayotoa virutubisho vya mimea ambavyo vinaboresha mazingira ya mimea na kuhakikisha afya bora ya mimea ya udongo na rutuba na kuongeza uwezo wa mmea kufyonza virutubisho kutoka aridhini na kupelekea mkulima kupata mazao lengo likiwa ni kuleta matokeo chanya kwa wakulima ikiwa ni pamoja na kufanya kilimo chenye tija.
Kampuni hiyo iliyopewa kibali kutoka Serikalini kuzalisha mbolea ya Ruzuku ndani ya nchi imetoa semina kwa wadau mbalimbali wa kilimo pamoja na wauzaji na wasambazaji wa pembejeo za kilimo Mkoa wa Arusha ili kuwapatia elimu juu ya faida na matumizi ya mbolea hiyo, semina iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano Golden Rose jijini Arusha.
Akizungumza wakati wa semina hiyo, Mkurugenzi wa biashara na masoko wa kampuni hiyo, keneth Masuke, amesema kuwa, lengo la kuanzisha uzalishaji wa mbolea hizo ni kumfanya mkulima aweze kulima kwa tija kutokana na sababu kuwa mbolea hizo zina mseto wa mbolea za asili ikiwemo samadi na mbolea za chumvichumvi hali itakayopelekea ardhi kudumu kwa muda mrefu na kuendelea kuzalisha mazao kwa wingi.
“Tumejikita sana na uboreshaji wa afya ya udongo kwa kulinda viumbe hai wanaoishi ardhini kwa kuwa ardhi ina uhai, hivyo kwa kufanya hivyo itamsaidia mkulima kuvuna mazao kwa wingi na kumwinua mkulima kutoka kilimo cha mazoea hadi kilimo chenye tija.” Ameweka wazi Mkurugenzi Masuke.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Uthibiti wa matumizi ya mbolea (TFRA) Kanda ya Kaskazini, Gothard Liapawe ameisisitiza kampuni hiyo kuendelea kutoa elimu Zaidi kwa wakulima na kuhamasisha kilimo cha kutumia mbolea kitaalamu na kuondokana na kilimo cha mazoea kwa kuwa ardhi haina rutuba ya kutosha kutoa mazao mengi bila kutumia mbolea kutokana na kutumika sana kwa muda mrefu pamoja na mabadiliko ya tabia ya nchi.
“Hii ni fursa kubwa kwa wakulima kutumia mbolea hii ambayo ina mchanganyiko wa mbolea za asili ikiwemo samadi, niwatake wakulima wazingatie matumizi ya mbolea kwa viwango sahihi kama walivyoelekezwa na maafisa ugani ili waweze kuongeza rutuba katika ardhi zao sambamba na kuvuna mazao kwa wingi.” Amesisitiza Mkurugenzi Liapawe.
Hata hivyo, Dkt. Julius Nambua ambaye ni meneja masoko na biashara na utafiti kutoka kampuni ya Bens Agrostar Company Limited amesema kuwa uzalishaji wa mbolea hizo mpya ni tukio la kihistoria na zimekuja kwa wakati mwafaka wa kufanya ukombozi kwa mkulima kwa sababu uzalishaji wake ni wa kisasa Zaidi kwa kutumia virutubisho vya asili tofauti na mbolea zingine zilizozoeleka.
“Serikali imefanya jitihada kubwa sana kuhakikisha mbolea inapatikana kwa wakulima wote kutokana na sababu kuwa hivi karibuni Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizopata adha ya ukosefu wa mbolea kutokana na athari za UVIKO 19 pamoja na vita vya nchi za Urusi na Ukraine ambapo sasa tunajivunia Nchi yetu inaweza kujitegemea kwa uzalishaji wa mbolea zinazotosheleza mahitaji yote ya wakulima.
Naye Afisa kilimo halmashauri ya Arusha, Mhandisi Chrisbeln Saria, licha ya kuishukuru kampuni hiyo kwa kuibua aina hiyo ya mbolea ambayo imeongeza wigo wa upatikanaji ndani ya nchi, amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imelenga kuwapunguzia wakulima mzigo wa bei ya mbolea kupitia ruzuku na kuongeza uzalishaji wa mazao kwa wakulima kwa kujenga mazingira mazuri ya upatikanaji wa mbolea ndani ya nchi.
Aidha wakulima pamoja na wadau waliohudhuria semina hiyo wamefurahishwa na ujio wa mbolea hizo za ruzuku huku wakisema zimekuja kwa wakati mwafaka na kuishukuru serikali kwa kuendelea kuwashika mkono kwa kuwa mbolea hizo zitaleta ukombozi kwao.
“Tunaishukuru sana serikali kwa juhudi walizozifanya kwa kuhakikisha kuwa kiwanda hiki kinajengwa ndani ya nchi na sisi wakulima tunapata mbolea zenye ubora kwa urahisi tofauti na kuagiza nje ya nchi ambapo kunakuwa na usumbufu mkubwa ikiwemo mfumuko wa bei.” Amesema Abraham Lengai ambaye ni mkulima kutoka Kata ya Kiranyi, halmashauri ya Arusha.
Awali, kampuni hiyo ambayo imeanza uzalishaji wa mbolea za aina tatu, kupandia, kukuzia na kunenepesha mwishoni mwa mwaka jana inatarajia kuzalisha mbolea Zaidi ya tani milioni moja kwa mwaka ambazo zinaweza kukidhi mahitaji ya matumizi ya mbolea kwa wakulima wote ndani ya nchi na kuifanya Tanzania kuwa na jumla ya viwanda viwili vinavyozalisha mbolea ndani ya nchi.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍
Mkurugenzi wa biashara na masoko wa kampuni ya Itracom Fertilizers Limited, keneth Masuke akitoa ufafanuzi juu ya utengenezaji wa mbolea ya FOMI pamoja na manufaa yake kwa wadau mbalimbali wa kilimo pamoja na wauzaji na wasambazaji wa pembejeo za kilimo Mkoa wa Arusha.
Mgeni rasmi katika semina hiyo ambaye ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Uthibiti wa matumizi ya mbolea (TFRA) Kanda ya Kaskazini, Gothard Liapawe wakati akizungumza na wadau mbalimbali wa kilimo pamoja na wauzaji na wasambazaji wa pembejeo za kilimo.
Abraham Lengai ambaye ni mkulima kutoka Kata ya Kiranyi, halmashauri ya Arusha wakati akiuliza swali juu ya matumizi ya mbolea hiyo.
Dkt. Julius Nambua ambaye ni meneja masoko na biashara na utafiti kutoka kampuni ya Bens Agrostar Company Limited wakati akizungumza na wadau mbalimbali wa kilimo pamoja na wauzaji na wasambazaji wa pembejeo za kilimo.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.