Na Elinipa Lupembe
Shirika lisilo la kiserikali la Climate Change Solution (CCS) limejipanga kuanza kutekeleza mradi wa kuchuja maji ili kuondoa madini ya floride kijiji cha Engutukoit kata ya Oldonyowas.
Akiwasilisha mpango wa utekelezaji wa mradi huo, kwa wajumbe wa kikao cha menejiment, kwenye ofisi ya mkurugenzi mtendaji halamsahuri ya Arusha, Mratibu wa mradi, Jorg Lenkel amesema kuwa shirika hilo linatarajia kutekeleza mradi huo wa maji unaotarajia kugharimu kiasi cha shilingi milioni 71 fedha za kitanzania.
Amesema kuwa mradi huo utahusisha ukarabati wa miundombinu ya maji iliyopo kijijini hapo, ujenzi wa tanki lenye ujazo wa lita 5,000 litakalosimikwa mtambo wa kuchujia maji kupitia madini ya mkaa, pamoja na kiongeza vituo vya kuchotea maji kijijini hapo.
Jorg amesema kuwa lengo la mradi huo, kuweka mfumo utakaowezesha upatikanaji wa maji safi na salama kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kwa wakazi wa Engutukoit, kutokana na changamoto kubwa inayowakabili wananchi wa eneo hilo ya maji kuwa na kiasi kikubwa cha madini ya floraidi, madini ambayo yana madhara makubwa kwa binadamu.
Aidha amefafanua kuwa mradi huo unategemea kutekelezwa kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia sasa na unategemea kuhudumia wananchi wote wa kijiji cha Engutukoit.
Hata hivyo, menejiment ya halmashauri, imepokea kwa mikono miwili mradi huo kutokana na ukweli kuwa, maeneo hayo yana maji yenye kiasi kikubwa cha madini ya floraidi, madini ambayo yana athari kubwa kwa binadamu.
Kaimu mkurugenzi, halmashauri ya Arusha Omary Sembe, amewataka wadau hao kutekeleza mradi huo kwa kuzingatia viwango vya ubora unaoendana na thamani ya fedha, pamoja na kuzingatia kanuni, sheria na taratibu za nchi ikiwemo mila na desturi za wakazi wa eneo hilo.
Awali shirika la CCS linafanya kazi kwa kushirikiana na shirika la Oikos East Africa, na kutekeleza mradi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji Vijijini RUWASA - ARUMERU kwa ufadhili wa Free State of Saxony kupitia Foundation North South Bridges, the working Group wa nchini Ujerumani.
"ARUSHA DC ni Yetu, Tushirikiane Kuijenga"
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.