Na. Elinipa Lupembe.
Ubalozi wa japani nchini Tanzania, umeendelea kushiriki kuchangia sekta ya elimu halmashauri ya Arusha, wilaya ya Arumeru, kwa kujikita katika ujenzi wa miundo mbinu ya shule, ili kuweka mazingira rafiki ya kufundishia na kujifunzia kwa wanafunzi na kupandisha kiwango cha elimu nchini.
Ubalozi huo wa Japani, umefanikisha ujenzi wa msingi wa jengo la ghorofa mbili lenye jumla ya vyumba 12, kati ya vyumba hivyo, tayari vyumba vinne vya madarasa, matundu ya vyoo pamoja na meza na viti 160, katika shule ya sekondari Sokoni II, vimekamilika, kwa gharama ya shilingi milioni 196.
Akizungumza shuleni hapo jana, Afisa Miradi, Ubalozi wa Japani nchini Tanzania, Ayuni Sakai, amesema kuwa, amefurahishwa sana kuona jengo hilo limekamilika na wanafunzi wameanza kutumia madarasa hayo, jambo ambalo ndilo lengo hasa la ubalozi huo wa Japani nchini na kuahidi kuendelea kushirikiana na halmashauri hiyo, kutekeleza miradi mingine ya kijamii.
"Nimefurahishwa sana na ushirikiano wenu na ukamilishaji wa jengo hili, mmeonyesha jitihada kubwa kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa wakati na kwa ubora, nimefurahi zaidi kuona tayari wanafunzi wanafundishwa kwenye mazingira bora wakiwa na furaha pamoja na walimu wao" amesema Ayuni.
Ameongeza kuwa, lengo la Ubalozi huo ni kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kuboresha huduma za jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kwa ajili ya maendeleo ya nchi yao, na dunia kwa ujumla.
Nao wanafunzi wa kidato cha nne shule ya sekondari Sokoni II, wanaotumia madarasa hayo, wameushukuru Ubalozi huo wa Japani kwa msaada wa ujenzi wa vyumba vya madarasa, uliowawezesha kufundishiwa kwenye mazingira bora sasa, mazingira ambayo yamewarahisishia tendo zima la kujifunza na kufundishwa na wameahidi kufanya vizuri katika matokeo yao ya mtihani wa taifa wanaotegemea kufanya mwanzoni wa mwezi Novemba 2020.
Josephine Maglani, mwanafunzi wa kidato cha nne, amethibitisha kuwa, yeye na wanafunzi wenzake wanaupongeza Ubalozi huo, kwa kuwajengea madarasa, jambo ambalo ni la maendeleo makubwa shuleni kwao, na kuhaidi kuongeza bidii katika masomo na kupata ufaulu wa kiwango cha juu katika shule yao, kwenye mitihani yao ya Taifa mwaka huu.
"Mimi na wanafunzi wenzangu, tumefurahishwa na hatua hii ya kimaendeleo shuleni kwetu, kwa kuwa sasa, tunasoma kwenye madarasa mazuri na tunaahaidi kufanya juhudi na kufaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza na la pili" amesema Josephine"
Mkuu wa shule ya Sekondari Sokon II, mwalimu Mwamvita Kilonzo, licha ya kuushukuru Ubalozi huo wa Japani, amethibitisha kuwepo kwa changamoto kubwa ya uhaba wa vyumba vya madarasa shuleni hapo, changamoto inayotokana na ongezeko kubwa la wanafunzi, tangu serikali ya awamu ya tano, kuanza kutoa elimu bila malipo.
Ameongeza kuwa, mradi huo umesaidia kutatua changamoto ya uhaba huo, kwa kiasi kikubwa, kutokana na ukweli kwamba, Januari mwaka huu 2020, wamepokea jumla ya wanafunzi 314 wa kidato cha kwanza na endapo madarasa hayo yasingejengwa, wanafunzi hao wangekosa mahali pa kusomea.
" Kukamilika kwa madarsa haya, kumetusaidia sana kutatua changamoto ya uhaba wa madarasa, kwani hatukuwa na madarasa ya kutosha kwa ajili ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka huu.
Awali, ujenzi wa jengo hilo ulianza mapema mwezi Machi 2019 na kukamilika mwishoni mwa mwaka huo, hata hivyo ubalozi huo wa Japani, umekuwa na ushirikiano mkubwa wa kimaendeleo na halmashauri ya Arusha, mpaka sasa umeweza kujenga miundombinu ya shule za Sokoni II na Enyoito pamoja na ukamilishaji wa Kituo cha Afya Manyire.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.