Na Elinipa Lupembe
Wajumbe wa Kamati ya Fedha Utawala na Mipango, halmashauri ya Arusha, wamewapongeza wananchi wa Kimnyaki kwa kujitoa kuanza ujenzi wa bweni la wasichana shule ya sekondari Kimnyaki, lenye uwezo wa kulaza wanafunzi 80.
Pongezi hizo zimetolewa wakati wajumbe wa kamati hiyo walipofanya ziara ya kukagua shughuli za utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa robo ya kwanza mwaka wa fedha 2022/2023
Akiwasilisha taarifa ya mradi huo, mkuu wa shule ya sekondari Kimnyaki, Mwl Maria Chami, amesema kuwa mradi huo, ulianza kwa nguvu za wananchi kwa kufanya harambee na kupata jumla ya shilingi milioni 19 ambazo zilianza ujenzi wa msingi.
Mwalimu Maria amesema kuwa mradi huo uko katika hatua za awali na kukamilika kwakwe kunategemea kugharimu shilingi milioni 150.8, huku halmashauri imetoka shilingi milioni 10 kupitia mapato yake ya ndani, na kuahidi kuendelea kutoa fedha hizo kwa mujibu wa bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2022, fedha ambazo zitaongeza nguvu za kuendeleza ujenzi wa bweni hilo.
Naye Diwani wa kata ya Kimnyaki Mhe. Eliakimu Marivei, amebainisha kuwa, wananchi wa Kimnyaki waliamua kuunganisha nguvu kujenga bweni la wasichana shuleni hapo, kwa kuzingatia usalama wa mtoto wa kike anayekabiliwa na changamoto za vishawishi vinavyosababisha mimba na ndoa za utotoni.
"Tumeamua kujenga bweni, kumuwezesha mtoto wa kike kusoma na kutimiza ndoto zao bila vikwazo, kiwa ni utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kuboresha miundombinu ya elimu nchini". Amefafanua Mhe.
Hata hivyo wajumbe wa kamati ya fedha wamepongeza wananchi wa Kimnyaki pamoja kurudhishwa na maendeleo ya ujenzi, na kumuagiza mkurugenzi wa halmashauri kuendelea kutoa fedha kwa mujibu wa bajeti ili kuunga mkono juhudi za wananchi wa Kimnyaki.
Makamu Mwenyekiti Halmashauri ya Arusha, Mhe. Selina Mollel, amewapongeza wananchi wa kata ya Kimnyaki kupitia Mheshimiwa Diwani wao, na kuwataka wengine kuiga mfano huo na kuwataka madiwani kuunga mkono juhudi hizo kwa manufaa ya wasichana na wananchi wa halmashauri ya Arusha.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.