MABADILIKO YA MRADI WA UJENZI WA MADARASA NA VYOO KUTOKA SHULE YA MSINGI KIYOGA KWENDA SHULE YA MSINGI OLOKII KATA YA BWAWANI
Mkurugenzi Mtendaji, Halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, anautaarifu Umma, kutokea kwa mabadiliko ya mradi uliokuwa utekelezwe kwenye shule ya Msingi Kioga kata ya Ilkiding’a na kuhamishiwa shule ya msingi Olokii Kijiji cha Olmapinu kata ya Bwawani.
Aidha Mkurugenzi Msumi amezitaja sababu za kuhamishwa kwa mradi huo ni baada ya Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI kujiridhisha kuwa shule hiyo haina eneo la kutosha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo.
Fedha za mradi huo ZIMEPELEKWA shule ya Msingi Olokii badala ya shule ya Msingi Kioga kama ilivyokuwa imepangwa hapo awali kwa kuzingatia taratibu za kuhamisha Miradi kupitia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha na Ofisi ya Rais TAMISEMI na tayari fedha hizo zimeanza kutekeleza Mradi katika shule ya Msingi Olokii Kata ya Bwawani.
Ikumbukwe kuwa mapema mwezi Machi, 2023, Halmashauri ya Arusha ilipokea kiasi cha shilingi milioni 682.5 kutoka Serikali Kuu, kupitia Mradi wa Kuboresha Upatikanaji wa fursa sawa katika Ujifunzaji bora kwa Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu kwenye shule 6 za msingi za halmashauri ya Arusha.
Katika mgao huo shule ya Msingi Kioga ilipangiwa fedha, kiasi cha shilingi milioni 81.3 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa na matundu manne ya vyoo.
Mradi wa BOOST unatekelezwa nchini kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026 ambayo itahusisha ujenzi wa shule mpya, madarasa na ukarabati wa miundombinu ya shule za msingi.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.