Katika kuendelea kukabiliana na vitendo na matukio ya ukatili dhidi ya watoto, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, imefanya maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika kwa njia ya pekee kwa kuwashirikisha watoto waliokumbana na changamoto ya matukio ya ukatili ikiwemo kukeketwa, kuchumbiwa wangali shuleni na wengine kuozeshwa.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya chuo cha ufundi stadi Mwandeti kata ya Mwandeti huku watoto hao wakitoa kilio chao kwa serikalo juu ya kuimarisha ulinzi juu yao, kuanzia ngazi ya familia na jamii kwa ujumla.
Watoto hao wamewataka wazazi kutambua na kuthamini haki zao na zaidi kuimarisha miundo mbinu ya ulinzi dhidi ya ukatili unafanyika ndani ya familia na jamii kwa ujumla.
Akizingumza wakati wa sherehe hizo, mgeni rasmi na mkurugenzi mtendaji, halmashauri ya Arusha Dkt. Wilson Mahera amesema kuwa halmashauri imejipanga kuhakikisha watoto wanalindwa dhidi ya ukatili na kuwataka wazazi na jamii nzima kushiriki kuwalinda watoto.
Ameongeza kuwa licha ya mila na desturi potofu za jamii ya wenyeji wa maeneo hayo zinafanya kwa siri ukeketaji lakini mkurugenzi huyo ameitaka jamii kuacha mara moja tabia hiyo na kuwataka watoto kutoa taarifa pale wanapofanyiwa au kutaka kufanyiwa ukatili wa aina wowote.
Hata hivyo, mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali yanayofanyakazi katika halmashauri hiyo, wametangaza kushirikiana na Serikali katika kupata muarobaini wa matukio ya ukatili yanayowakabili watoto, ndani ya halmashauri hiyo.
Baadhi ya mashirika yasiyo ya kiserikali ya Ace Africa na WDCD wamejikita kwenye uwezeshaji watoto katika shule kwa kuanzisha klabu shuleni ambazo zinawawezesha watoto kutambua haki na wajibu wao, pamoja na kutoa taarifa pale wanapofanyiwa ukatili.
Aidha wadau hao, wamewataka watoto kutumia mbinu na stadi za maisha wanazopewa, kwa kuwa mbinu hizo zitawawezesha watoto hao kujitambua, kujisimamia pamoja na kukua katika maadili, yanayowawezesha kujitegemea na kujiajiri katika sekata ya kilimo na viwanda.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.