Na Elinipa Lupembe.
Kufuatia mkakati wa serikali wa kuboresha miundombinu ya shule zake za serikali, halmashauri ya Arusha, imeendelea kutekeleza mkakati huo kwa kuendelea kukamilisha ujenzi na ukamilishaji wa maabara za mamsomo matatu ya Sayansi katika shule za sekondari ya kata.
Mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka huu wa fedha 2020/2021, halmashauri hiyo inategemea kufikisha jumla ya maabara 78 za masomo ya Sayansi kati ya maabara 99 zinazohitajika katika shule 33 za sekondari za serikali na kufikia asilimia 80 ya kila shule ya sekondari kuwa na maabara tatu za masomo ya Sayansi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Afisa Mipango, halmashauri ya Arusha Anna Urio, amesema kuwa mpaka sasa, katika kukamilisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2020/2021, halmashauri imepokea jumla ya shilingi milioni 210, kwa ajili ya ukamilishaji wa maabara 7 katika shule saba za sekondari za kata, na kuongeza kuwa ujenzi wa maabara hizo unaendelea vema na unategemea kukamilika mwishoni mwa mwezi Julai,202.
Amefafanua kuwa kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu na vifaa vya maabara hizo za shule saba, kutafikisha jumla ya maabara 78 kati ya maabara 99 zinazohitajika kwa shule 33 za sekondari za serikali katika halmashauri ya Arusha
"Serikali inaendelea kutekeleza mkakati wake wakuboresha miundombinu ya elimu kwa kuhakikisha kila shule ya sekondari inakuwa na maabara tatu za masomo ya Sayansi, jambo ambalo linatekelezeka kwa kasi katika halmashauri yetu ya Arusha. Amesema Afisa Mipango huyo.
Naye Kaimu Afisa Elimu, halmashauri ya Arusha, Safi Mturi, amesema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu ya maabara hizo, licha ya kurahisisha tendo la kujifunza na kufundisha kati ya mwalimu na mwananfunzi zaidi, kutasaidia ongezeko la idadi ya wanafunzi kujikita kwenye masomo ya Sayansi, kutokana na uhalisia ya kuwa, masomo ya Sayansi yanahitaji mafunzo kwa vitendo zaidi, na kuvutia wanafunzi kujifunza.
Kaimu Afisa Elimu huyo, ameweka wazi kuwa, katika shule za sekondari za kata, idadi ya wanafunzi wanaosoma masomo ya Sayansi inaendelea kuongezeka siku hadi siku, kutokana na uwepo wa maabara za masomo ya Sayansi, jambo linaloaminika kuwa maabara hizo zinachochea kasi ya uwelewa wa masomo hayo kwa wanafunzi.
"Maabara hizo za Sayansi zitafanya mapinduzi katika shule za kata, na kuongeza idadi ya ndogo ya wanafunzi wanaosoma masomo ya Sayansi, kulinganisha na idadi ya kubwa ya wanafunzi wanasoma masomo ya sanaa kitokana na uhaba wa maabara za masomo ya Sayansi, uliokuwepo hapo awali" amefafanua Kaimu Afisa Elimu.
Hata hivyo baadhi ya wakuu wa shule za sekondari halmashauri ya Arusha, wamethibitisha kuwa, ujenzi wa maabara za masomo ya Sayansi katika shule za sekondari, kutaongeza ari ya wanafunzi kujiunga na masomo ya Sayansi pamoja na kuyapenda masomo hayo, masomo ambayo hapo awali wanafunzi wengi waliamini kuwa ni magumu.
Naye mkuu wa shule ya sekondari Musa, mwalimu Gilbert Kafunafu, amesema kuwa uwepo wa maabara za masomo ya Sayansi katika shule yake, licha ya kusaidia kurahisisha tendo la kujifunza na kufundisha kwa walimu na wanafunzi, maabara zitaongeza idadi ya wanafunzi kujiunga na masomo ya Sayansi tofauti na hapo awali.
"Katika Shule yangu licha ya changamoto wa uchache wa walimu wa masomo ya Sayansi, kulikuwa na mwamko mdogo wa wanafunzi kujiunga kwenye masomo ya Sayansi tofauti na masomo ya sanaa, hii ni kutokana na ukosefu wa maabara za kufanyia mafunzo kwa vitendo, ninaamini sasa uwepo wa maabara za masomo yote matatu ya Sayansi kutaongeza ari na idadi ya wanafunzi watakaojiunga na mchepuo wa Sayansi" amethibitisha Mkuu huyo wa shuke.
Mwalimu huyo ameweka wazi kuwa, shule ya Sekondari Musa imepata kiasi cha shilingi milioni 30, kwa ajili ya kumalizia maabara ya somo la Kemia, na kuongeza kuwa maabara hiyo itakamilisha maabara tatu za masomo ya Sayansi katika shule hiyo, masomo ya Bailojia , Fizikia na Kemia.
Awali halmashauri ya Arusha imepokea kiasi cha shilingi milioni 210 kutoka Serikali Kuu, kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi na ukamilishaji wa maabara 7 za masomo ya Sayansi katika shule za sekondari Bangata, Einoti, Losinoni, Musa, Oljoro, Olturumet na Sambasha zikiwa zote ni shule za Kata.
ARUSHA DC
Kazi inaendelea ✍✍
Jengo la maabara ya somo la Kemia shule ya sekondari Musa
Jengo la maabara ya somo la Kemia shule ya sekondari Einoti
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.