Na Elinipa Lupembe
Mkuu wa wilaya ya Arumeru, Mhe. Emmanuela Mtatifikolo Kaganda, amefungua mkutano wa tathmini wa mwaka wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali (NGO's) kwa mwaka 2022, halmashauri ya Arusha, mkutano unaofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
Akifungua mkutano huo, Mhe. Emmanuela licha ya kutambua, kushukuru na kuthamini kazi zinazofanywa na mashirika hayo, ameyataka mashirika hayo kufanyakazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu na miongozo ya nchi hasa kwa kutekeleza miradi inayozingatia vipaumbele vya maendeleo vya Taifa pamoja na kuzingatia maadili, mila na desturi za kiTanzanzia.
"Tunataka mashirika kutekeleza miradi inayotoa hudma za jamii na kwa kuzingatia vipaumbele vya Taifa, na si vinginevyo, tunatambua changamoto nyingi zinazowakabili wananchi wetu lakini miradi hiyo izingatie vigezo vya Taifa na maendeleo ya jamii husika". Amefafanua Mhe. Emmanuela.
Aidha ameyataka mashirika hayo kufanya kazi kwa uwazi kwa kushirikiana na watalamu na viongozi wa ngazi zote kuanzia ngazi ya wilaya, halmashauri, kata, vijiji na vitongoji pamoja na kuwashirikisha wananchi wa maeneo ambayo miradi inayotekelezwa.
Zaidi Mkuu wa wilaya huyo ameyasisitiza mashirika hayo kufanya kazi kwa uwazi kwa kuitambulisha miradi hiyo na kuhakikisha wananchi wanaifahamu vizuri miradi inayotekelezwa katika maeneo yao, gharama za mradi, muda wa utekelezaji pamoja na kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa miradi hiyo kila robo ya mwaka kwa idara husika.
"Hatutasita kuyachukulia hatua za kisheria mashirika yote yasiofuata taratibu za serikali, yapo mashirika yasiyowasilisha taarifa kulingana na taratibu na maelekezo ya serikali kwa kila robo, mashirika hayo tutayashughulikia kwa mujibu wa sheria, Niyatake mashirika yote kufuata taratibu". Amefafanua Mkuu huyo wa Wilaya.
Mkutano huo wa mwaka ni wa kisheria unalenga kupokea taarifa za utekelezaji wa shughuli za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO's) kuanzia Januari - Desemba 2022, wenye lengo la kufanya tathmini ya miradi ya iliyotekelezwa kwa mwaka.
ARUSHA DC ni Yetu, Tushirikiane Kuijenga"
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.