Hatimaye uendelezwaji wa ujenzi wa jengo la ghorofa moja, lenye vyumba sita vya madarasa shule ya sekondari Ilkiding'a umeanza baada ya ujenzi huo kusimama kwa muda mrefu.
Ingawa ujenzi wa jengo hilo ulianza rasmi miaka ya 2004 na kusimama kwa muda mrefu, Serikali ya awamua ya tano, kupitia kampeni ya TUNATEKELEZA imeweza kufanikisha uendelezwaji wa jengo hilo kupitia vyanzo mbalimbali vya fedha.
Akisoma historia ya jengo hilo, mkuu wa shule ya sekondari Ilkiding'a, mwalimu Ivan Mmari, amesema kuwa, jengo hilo lilianza kujengwa mwaka 2004 na kuachwa kwa muda, mwaka wa fedha 2016/17 ujenzi umeanza baada ya halmashauri kutoa fedha kiasi cha shilingi milioni 40 kwa awamu mbili.
Mkuu huyo wa shule amefafanua kuwa, mpaka sasa vyumba vitatu vya sakafu ya chini vimekamilika kwa zaidi ya asilimia 70, na kuongeza kuwa ukamilishaji jengo hilo la ghorofa unahitaji jumla ya shilingi milioni 243.
Hata hivyo Mwalimu Mmari, ameendelea kueleza kuwa, kwa awamu ya kwanza, vyumba vitatu vya madarasa vitakamilika na kukamilika kwa vyumba hivyo kutapunguza msongamano mkubwa wa wanafunzi madarasani, unaikabili shule hiyo kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi wanaosoma shuleni hapo.
Diwani wa kata ya Ilkiding'a mheshimiwa Loth Mungaya amesema kuwa, katika ujenzi unaoendelea sasa, wananchi wa Ilkiding'a wamechangia shilingi milioni 4.1, fedha ambazo zinatumika kulipia gharama za ufundi.
Diwani huyo, amesisitiza kuwa wananchi wa Ilkiding'a wamekuwa wakijitoa kwa hali na mali, kuchangia maendeleo ya shule hiyo, kwa kutambua kuwa shule ni mali yao na kuhakikisha watoto wao wasome katika mazingira bora yenye ushawishi wa kujifunza.
Hata hivyo halmashauri imepanga kutoa milioni 60 kwa mwaka huu wa fedha, na kuendelea kuweka kwenye bajeti kwa miaka ijayo ya fefha, mpaka sasa halmashauri imeshatoa shilingi milioni 40, ikiwa milioni 20 ni fedha za programu ya Lipa Kutokana na Matokeo 'P4R'.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.