Na Elinipa Lupembe.
Jamii imetakiwa kuachana na dhana potofu za kudhani kuwa chanjo na kinga tiba zinazotolewa na serikali zina madhara kwa afya ya binadamu na kushawishi wengine kukataa.
Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Arusha, Mhe. Ojung'u Salekwa, wakati akizindua zoezi la kitaifa la umezeshaji vidonge vya kinga tiba dhidi ya minyoo tumbo kwa watoto wa umri wa miaka 5 mpaka 14 halmashauri ya Arusha, uzinduzi uliofanyika kwenye shule ya msingi Olgilai kata ya Kiutu.
Mhe. Ojung'u amesema kuwa chanjo na kinga tiba zinazotolewa na serikali zikiwa zimepimwa na kuthibitishwa kuwa na viwango vya ubora kwa binadamu zaidi ni salama kwa afya za binadamu.
"Serikali inathamini afya za watanzania, na inaweka mipango thabiti ya kuwakinga wananchi hususani watoto dhidi ya magonjwa ambayo yana kinga, kwa kuwa kinga ni bora kuliko tiba".Amesema Mhe. Mwenyekiti.
Katika zoezi hilo Diwani wa kata ya Kiutu, ameishukuru serikali kwa kutoa kinga tiba hiyo ambayo inawakinga watoto dhidi ya minyoo tumbo ambayo ina madhara makubwa kwa afya ya binadamu hususani watoto.
Mganga Mkuu halmashauri ya Arusha, Dkt. Petro Mboya, amesema kuwa vidonge vinavyotolewa ni almebendazole ambavyo hukinga dhidi ya minyoo tumbo na hutolewa kwa watoto kwa sababu wako kwenye hatari ya kupata mayai ya minyoo kutokana na tabia za michezo ya watoto.
"Tunatoa kinga tiba kwa watoto wa miaka 5 mpaka 14 kwa kuwa wako kwenye hatari ya kupatwa na mayai ya minyoo, kutokana na uwezo wao mdogo wa kujikinga na uchafu, watoto wengi hushindwa kunawa mikono na hula bila kunawa mikono na wakati mwingine huokota vitu na kula". Amebainisha Dkt. Mboya
Mwalimu mkuu shule ya Msingi Oligilai, Mwl. Recho Kisiri, amesema kuwa, wanafunzi wamehudhuria masomo kwa wingi wao na wanategemea kumezesha dawa za minyoo takriban watoto 782 na kufikia asilimia 100.
Hata hivyo mratibu wa Magonjwa yasiyopewa Kipaumbele, Halmashauri ya Arusha, Ramadhani Kulewa, amesema kuwa, dawa tiba hiyo inatolewa kwenye vituo 211, shule za msingi 155, vituo vya afya 56, huku wahudumu 433 wakigawa dawa hiyo ambapo walimu ni 310 na wahudumu wa afya 112.
Awali Halmashauri inategemea kuwapatia kinga tiba ya minyoo kwa watoto elfu 80, watoto elfu 76 kati yao ni wale waliosajiliwa shuleni na watoto elfu 4 ni ambao hawajasajiliwa kwenye mfumo rasmi wa elimu.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍
Mwenyekiti halmashauri ya Arusha Mhe. Ojung'u Salekwa, akimmezesha dawa mwanafunzi wa shule ya msingi Olgilai, wakati wa kuzindua zoezi la chanjo ya kinga tiba ya minyoo tumbo
Diwani wa kata ya Kiutu Mhe. Malaki Malambo, akimmezesha dawa mwanafunzi wa shule ya msingi Olgilai, wakati wa kuzindua zoezi la chanjo ya kinga tiba ya minyoo tumbo
Afisa Mipango Msaidizi Kitengo cha Magonjwa yasiyopewa Kipaumbele Wizara ya Afya Dkt. Dorca Burengelo, akimmezesha dawa ya minyoo mwanafunzi wa shule ya msingi Olgilai kata ya Kiutu, wakati wa uzinduzi wa zoezi la Kitaifa la kumezesha dawa za kinga tiba dhidi ya Minyoo halmashauri ya Arusha.
Mganga Mkuu, Halmashauri ya Arusha, Dkt. Petro Mboya akimmezesha dawa ya minyoo mwanafunzi wa shule ya msingi Olgilai, wakati wa uzinduzi wa Zoezi la kitaifa la kumezesha dawa za kinga tiba dhidi ya Minyoo halmashauri ya Arusha.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.