Mwenyekiti wa Halmshauri ya Arusha Mhe. Dkt.Ojung'u Salekwa ameitaka Jamii ya Watanzania kuendelea kushirikiana katika suala malezi ya watoto pasipo kubagua jinsia ya mtoto ili kuwa na Taifa lenye Afya.
Amezungumza hayo leo wakati wa kikao kazi cha Wadau kilichoandaliwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Center For Women and Children Center (CWCD) katika mradi wake wa kuwawezesha Watoto wa Kiume dhidi ya ukatili wa kijinsia.
Dkt.Salekwa amesema kuwa, jamii ya kitanzania lazima ichukue hatua za makusudi katika suala la malezi ya watoto kwani takwimu zinaonyesha kuwa wazazi wengi wamekuwa wakiwaacha watoto kujiamulia mambo yao wanavyotaka pasipo kukemewa.
"Utakuta mtoto mbele ya wazazi wake anavaa mavazi yasiyo na staha, lakini hakemewi na wazazi wanaona ni kwenda na usasa, hii inatuharibia Taifa kwani watoto hawa ndiyo Viongozi na wazazi wa wakati ujao", amesema.
Akizungumzia mafanikio ya mradi huo, mratibu wa Mradi kutoka Shirika la CWCD Epiphania Josephat amesema kwa kushirikiana na Halmshauri ya Arusha, wamefanikiwa kuanzisha maabara 6 za watoto wa kiume katika Shule za Msingi za Kiranyi, Moivo, Naurei, Ngaramtoni, Ilboru na Oltruroto. Vilevile wameteua baba waangalizi 6 kwa kila kata, pamoja na vikundi 6 vya malezi kwa kila Kata.
Kupitia vikundi hivyo, Shirika la CWCD kwa kushirikiana na Halmshauri ya Arusha, wameweza kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo watoto wa kiume ili wajitambua katika kuzijua haki zao pamoja na kuripoti vitendo vyovyote vya ukatili wa kijinsia vinavyoendelea katika jamii wanazotoka.
Kwa upande wake, Afisa Ustawi wa Jamii Halmshauri ya Arusha Beatrice Tengi amesema kuwa, Serikali imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la CWCD katika mpango wa makuzi ya mtoto kuanzia ujauzito mpaka miaka 8 ikiwa ni kumjenga mtoto kimakuzi kwa kuhakikisha mtoto anapata malezi salama ikiwemo elimu bora.
Akifunga Kikao hicho, Mkurugenzi wa Halmshauri ya Arusha DC, Seleman Msumi amesema kuwa, Serikali imeweka mkazo katika kuhakikisha inamlinda mtoto dhidi ya vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa kufungua madawati ya kushughulikia vitendo hivyo ndani ya Jeshi la Polisi.
Vilevile Msumi ametoa wito kwa Viongozi wa Dini, kuendelea kutoa mafundisho katika nyumba za Ibada ili jamii iweze kuwa na hofu ya Mungu, kwani pasipo kufanya hivyo Taifa litakosa nguvu kazi ya baadaye ambayo inategemea sana Vijana.
ARUSHA DC NI YETU, TUSHIRIKIANE KUIJENGA
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.