Katika kuendelea kuzikwamua kaya masikini hapa nchini, Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii - TASAF, imeendelea kuwajengea uwezo wa kiuchumi wananchi walio kwenye Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini, kupitia mradi wa OPEC III.
Halmashauri ya Wilaya ya Arusha kupitia mradi kupitia mradi huo wa OPEC III umegawa kuku 750 kwa kaya masikini 75 mradi wenye thamani ya shilingi milioni 37 kwenye kijiji cha Oldonyowas kata ya Oldonyowas.
Akizungumza wakati wa zoezi la kuwakabidhi kuku hao, Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha Dkt. Wilson Mahera amezitaka kaya hizo kutunza mradi huo wa kuku ili uweze kuwakwamua kiuchumi, kwa manufaa yao na jamii kwa ujumla.
Aidha amewataka wananchi hao, kuwatumia watalamu wa mifugo walio kwenye kata yao, kupata maekekezo ya kufuga kitalamu na kisasa na kuwasisitiza watalamu wa mifugo kuhakikisha wanawasimamia wafugaji hao ili mradi huo uweze kuwa endelevu.
Naye Kaimu Mratibu wa TASAF , Grace Makema amesema kuwa, mradi huo umegawa kuku 750 kwa kaya masikini 75 kwa mgao wa kuku 10 kila kaya, mradi ambao umeibuliwa na wanakaya wenyewe.
Ameongeza kuwa wanakaya hao kabla ya kuibua miradi huo walipatiwa mafunzo ya ujasiriamali, na baada ya kuibua miradi yao wamepatiwa pia mafunzo ya namna ya kuendeleza mradi huo na tayari mtalamu wa mifugo yuko karibu nao kwa ajili ya kuwaelekeza namna bora ya ufugaji wa kuku.
Naye Diwani wa kata ya Oldonyowasi, mhe. Elisante Nasari amekiri kuwa, mradi wa TASAF unawawezesha wananchi wake kujikwamua kutoka kwenye lindi la umasikini waliokuwa nao hapo awali.
" Mradi wa TASAF umewasaidi wananchi wangu, kujikwamua kiuchumi, kwa sasa angalau wengi wao wameanza kujitegemea na kujikimu na hali ya maisha ukilinganisha na kabla ya mpango huu kuwepo" amesema mheshimiwa Diwani.
Nao wanufaika wa mradi huo, hawakuwa nyuma kuishukuru serikali ya awamu ya tano kwa kuwajali wao na kutambua umuhimu kuwakwamua kiuchumi na kuahidi kuiendezela miradi hiyo ili waondokane kabisa na umasikini waliokuwa nao.
Anande Pinisi mmoja wa wanufaika hao licha ya kuishukuru serikali amepanga kuendeleza mradi huo wa kuku na baada ya muda kuanzisha mradi wa mbuzi ambao anaamini utamtoa kwenye umasikini aliokuwa nao.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.