Maafisa Watendaji wa kata na vijiji halmashauri ya Arusha wametakiwa kufanya kazi ya kuwahudumia wananchi kwa weledi kwa kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa Umma.
Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, halmashauri hiyo, Elizabeth Ngobei wakati wa kikao kazi cha kukumbushana maadili ya utumishi wa umma sambamba na utekelezaji wa majuku ya kazi, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa halmashauri hiyo.
Mkuu huyo wa Idara licha ya kuwapongeza kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuwahudumia wananchi katika maeneo yao, amewakumbusha kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu hasa kwa kuzingatia Sheri, Kanuni, taratibu na maelekezo maalumu ya Serikali.
"Kila mtu anaomuongozo wa majukumu anayopaswa kutekeleza kila siku, kila mtu anafahamu sheria, kanuni na taratibu za kazi lakini zaidi zingatieni na kutekeleza maagizo yanayoshushwa kwenu, kwa kutoka ofisi ya mkurugenzi, kwa kutambua kuwa mnaowajibu wa kufanyakazi kwa niaba ya mkurugenzi katika maeneo yenu" Amesisitiza Elizabeth.
Uwazi na uwajibikaji ndio nguzo kuu ya Utumishi wenu, ni wajibu kisheria kufanya vikao na mikutano ya kisheria kwa kila robo ya mwaka, inayotoa fursa kwa viongozi na wananchi kujadili taarifa za maendeleo ya kata na vijiji pamoja na kuwasomea taarifa za miradi ya maendeleo na taarifa za mapato na matumizi ya vijiji.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Fedha, CPA David Rubibira amewakumbusha watendaji hao kuongeza kasi ya kukusanya mapato pamoja na kuzingatia matumizi sahihi ya fedha hizo za Umma, yaliyoainishwa kwenye miongozo ya Serikali.Ameongeza kuwa vipo vyanzo vya mapato kwenye maeneo yenu, mkiwa kama wasimamizi wa mapato na matumizi ya fedha hizo, hakikisheni zinakusanywa kwa kutumia mashine za kukusanyia Mapato 'POS' na kuweka benki fedha hizo mara baada ya kukusanya na sio kutumia kabla ya kuziweka benki.
"Mnayo dhamana ya kusimamia Mapato na Matumizi katika maeneo yenu, ni vema kutambua kuwa, ni kinyume cha Sheria kukusanya fedha za Umma bila mashine ya 'POS' pia ni kosa kukaa na fedha hizo zaidi ya saa 24 bila kuziweka benki zaidi ni kinyume cha sheria kutumia fedha hizo kabla ya kuziingiza kwenye mfumo wa benki" Amesisitiza Mweka Hazina huyo.
Hata hivyo Mkuu wa Kitengo cha Ugavi, Hilda Mwangamila naye amewakumbusha suala zima la usimamizi wa fedha za miradi ya maendeleo hususani kwenye kipengele cha manunuzi, kwa kuwataka kuzingatia sheria za utekelezaji wa miradi kupita 'force Akaunti na matumizi ya 'local fundi', miradi ambayo kwa sasa Serikali imeelekezwa kutekelezwa kwenye ngazi za Kata na Vijiji.
"Manunuzi mnayoyafanya ni lazima yapitishwe na wajumbe wa kamati za ujenzi kupitia mzabuni aliyechaguliwa, na kuhifadhi nyaraka zote za manunuzi ikiwemo risiti, kuweni na faili za miradi kwenye ofisi zenu, wasilianeni na ofisi ya manunuzi katika hatua zote, ili kuepuka na kuondokana na hoja za ukaguzi na malamiko ya wananchi". Amefafanua Afisa Manunuzi huyo
Hata hivyo Maafisa Watendaji hao, wameushukuru uongozi wa Halmashauri kwa kikao kazi hicho chenye tija na kuahidi kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma ili kufikia malengo ya Serikali ya kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.
"ARUSHA DC Ni Yetu, Tushirikiane Kuijenga"
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.