Na Elinipa Lupembe
Waheshimiwa Madiwani wa kata 6 za halmashauri ya Arusha, wameahidi kushirikiana na shirika la CWCD kutekeleza mradi wa kumtetea Mtoto wa Kiume, ulioanza kutekelezwa kwenye shule sita ndani ya kata zao na kuahidi kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya mtoto wa kiume katika jamii.
Waheshimiwa hao, wamefikia maamuzi hayo, mara baada ya kushiriki kikao kazi cha kuutambulisha mradi huo, unaojulikana kama 'Boy's Vac Lab', unaofadhiliwa na Foundation for Civil Society, wenye lengo la kumjengea uwezo mtoto wa kiume wa kujitambua, kujithamini ili kupambana na ukatili dhidi yake.
Akizungumza wakati akiutambulisha mradi huo, Mkurugenzi wa shirika la CWDC, mama Hindu Mbwego, ameeleza kuwa shirika limeanzisha mradi huo, baada ya kuthibitika matukio mengi ya ulawiti kwa watoto wa kiume, na kugundua kuwa jamii ilielekeza nguvu kumlinda mtoto wa kike na kumsahau mtoto wa kume na madhara yake yameanza kuonekana sasa.
"Tafiti zinaonesha, matukio ya ulawiti kwa watoto wa kiume zimeongezeka kwa kasi, na kugundua kuwa kuna haja ya kuanza kuelekeza nguvu za kumlinda mtoto wa kiume kama ilivyo mtoto wa kike, kwa kuwa wote wanahitaji ulinzi, niwatake waheshimiwa madiwani tuungane kupaza sauti". Amesisitiza Mama Hindu
Aidha Madiwani hao, licha ya kulipongeza shirika hilo, wameeleza hisia zao juu ya kasi ya ongezeko la vitendo vya ulawiti kwa watoto wa kiume, na kuongeza kuwa jamii inatakiwa kugeuka na kuanza kupaza sauti juu ya matukio hayo.
Wamebainisha kuwa, kwa muda mrefu jamii ilielekeza nguvu, kumtetea mtoto wa kike na kumuacha kando mtoto wa kiume, jambo ambalo limesababisha watu waovu kuhamia kwa watoto wa kiume.
Mwenyekiti halmashauri ya Arusha na Diwani wa kata ya Laroi, amethibitisha kuwepo na ongezeko la ulawiti kwa watoto wa kiume nchini, ulawiti ambao wanafanyiwa na watu wa karibu wanaowaamini na mbaya zaidi watoto hao huanza kufanyiana wenyewe kwa wenyewe.
"Inasikitisha sana, matukio mengi yanayoripotiwa kwa sasa ni watoto wa kiume kulawitiwa na kulawitiana wenyewe kwa wenyewe, sisi kama viongozi, kupitia mradi huu, tumejipanga kutumia majukwaa mbalimbali kuelimisha jamii dhidi ya madhara ya vitendo vya ulawiti kwa watoto wa kiume".Amesesitiza Mwenyekiti Ojung'u
Diwani wa kata ya Kiranyi, Mhe. John Seneu, ameitaka jamii kufumbua macho sasa juu ya matukio hayo kwa watoto wa kiume, na kuungana kupambana nayo, kuanzia nyumbani, shuleni, makanisani, masokoni ili kuokoamkizazi cha watoto wa kiume.
"Inatia uchungu kuona vitendo hivi vinafanywa na watu tunaowaamini, viongozi wa dini, baba, mwalimu, kaka na mjomba!, ifike mahali sasa tupaze sauti kwa pamoja kukemea vitendo hivyo ni kinyume pia na maadili ya dini zetu". Ameeleza kwa hisia kali Mheshimiwa Seneu.
Naye Makamu Mwenyekiti halmashauti ya Arusha, Mhe. Selina Mollel, amewataka wazazi na walezi, kutambua kuwa jukumu la malezi ni lao, na sio kuiachia jamii, kila mzazi anawajibu wa kumtunza na kumlinda mtoto wake, waache tabia ya kumuamini mtu yoyote juu ya watoto wao kwani watoto wanalawitiwa na watu wa karibu wanaowaamini.
"Wazazi wamejisahau, wamekuwa bizy na kutafuta maisha, lakini fungueni akili anzeni kuwafuatilie watoto wenu popote walipo kuanzia nyumbani, shuleni na hata kanisani, tumeshudia Padri amelawiti watoto, watoto wanalawitiana wenyewe kwa wenyewe, inatia uchungu sana wakati umefika tuamke sasa" Amefafanua Mhe. Selina
Awali shirika la CWCD, linatekeleza miradi ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto kwenye kata 19 za halmashauri ya Arusha, huku mradi wa 'Boy's Vaccum Lab' ukitekelewa kwenye shule 6 za msingi za Moivo, Naurei, Olturoto, Ilboru, Kiranyi na Ngaramtoni kwa ufadhili wa shirika Foundation for Civil Society.
ARUSHA DC
KaziInaendelea ✍✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.