Na Mwandishi Wetu
Baada ya mateso ya muda mrefu ya changamoto ya upagikanaji wa maji, hatimaye wananchi wa kijiji cha Samaria kata ya Nduruma, Halmashauri ya Arusha, wamepata neema ya kupata maji safi na salama, baada ya serikali kutoa milioni 30 za kukamilika kwa mradi huo wa maji.
Wananchi hao waishukuru serikali kwa kusadia kutekeleza mradi wa maji ya kisima, ambao tayari umeanza kuwanufaisha wananchi hao na kusahau tabu waliyoipata kwa kipindi kirefu, kwa kutumia muda mrefu kutafuta maji, hali iliyosababisha kuzorota kwa baadhi ya shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.
Wakizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo, wananchi wamekiri, kukamilika kwa mradi kumekuwa na faida kubwa kwa kuwa, umeondoa adha iliyokuwepo hapo hususani kwa kina mama ambao waliteseka kutafuta maji.
“Sasa tumefikia ukomo wa mateso ya kutafuta maji, wanawake wa Samaria, tunaishukuru Serikali kwa kutushika mkono na kukamilisha mradi, upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama hasa umetuondolea kero kubwa kinama, tunaamini Serikali itaendelea kutusaidia ili maji yafike katika maeneo yote ya kijiji cha Samaria”. Alisema Damari Nnko Mkazi wa Samaria.
Hata hivyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi Mhe. Noah Lembris, ameweka wazi kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma za muhimu ikiwemo maji safi na salama ndani ya mita 400 huku akiwataka viongozi wa maeneo hayo kusimamia kwa uadilifu mradi huo ili kila mwananchi aweze kunufaika.
“Tunajipanga vyema namna ya kupanua na kuendeleza mradi huu kwa kusogeza huduma ya maji karibu na wananchi, niwaombe wananchi wa tuendelee kuwa wazalendo kwa mradi huu ili uweze kudumu kwa muda mrefu, shirikianeni na viongozi wa Serikali ya kijiji kuhakikisha mradi unawanufaisha wananchi wote”. Alisisitiza Mhe. Noah
Naye Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Arusha Seleman Msumi, ameishukuru familia iliyotoa eneo kwaajili ya kutekeleza mradi huo na kusisitiza kuwa kila mwananchi ana wajibu wa kutunza miundombinu iliyojengwa katika eneo hilo ili iendelee kuwasaidia wananduruma pamoja na vizazi vijavyo.
“Kwa kipindi kirefu kulikuwa na shida ya maji katika eneo hili, mama zetu walikuwa wanahangaika huku na kule kutafuta maji, mateso yalikuwa makubwa sana, lakini leo tunamshukuru Mungu kwa kukamilika kwa mradi huu, nawasihi kuendelea kutunza miundombinu hii ili iidumu na kuwahudumia wananchi wote”. Amesema Mkurugenzi Msumi.
Aidha Diwani Kata ya Nduruma Mhe. Raymond Mollel, amesema kutokana na historia ya eneo hilo ilisemekana kuwa hakuna uwezekano wa kupata maji katika Kijiji hicho, hivyo uwepo wa kisima hicho ni neema kubwa kwa wakazi wa Samaria.
Mradi wa kisima cha maji ulianza kutekelezwa kwa nguvu za wananchi baadaye Halmashauri ilitoa kiasi cha Milioni 30 fedha za mapato ya ndani na kukamilisha mradi huo.
ARUSHA DC
TUPO KAZINI✍✍
PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA UZINDUZI WA MRADI WA MAJI KITONGOJI CHA SAMARIA
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.