Na Elinipa Lupembe
Shirika lisilo la kiserikali la DSW, limekabidhi jengo kwa ajili ya Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa, halmashauri ya Arusha, kupitia mradi wa Binti na Maendeleo.
Akizungumza wakati wa kukabidhi jengo hilo Mkurugenzi wa DSW Tanzania Jan Kreutzberg, amesema kuwa, lengo la shirika ni kuhakikisha ukatili wa kijinsia unatokomezwa kwenye jamii kwa kuwajengea vijana uwezo wa kujitambua hasa wasichana wakiwa katika umri mdogo.
Mkurugenzi Jan, amebainisha kuwa, shirikia limefikia lengo la kuwa na Kituo mahali hapo, baada ya kuona matokeo chanya kwa wasichana wa kata ya Musa kupitia mradi wa Binti na Maendeleo, uliowezesha watoto kujitambua, kujithamini na kuanza kukataa kukeketwa na kuolewa katika umri mdogo na kusisitiza kuwa kituo hicho kitatumika, kuwapa mabinti eneo salama, la kujadiliana, kubadilishana uzoefu, kujifunza masuala mbalimbali ya ukatili wa kijinsia pamoja na elimu ya ujasiriamali ili kuwajengea uwezo wa kujikwamua kijamii, kiuchumi na kisaikolojia.
"Tunashirikiana na Serikali kuhakikisha ukatili wa kijinsia unatokomezwa katika jamii, kituo hiki kitakuwa kama mwongozo wa kusaidia mabinti wadogo ambao wako kwenye mazingira hatarishi ya kufanyiwa ukatili kwa kuwaunganisha na vituo vya huduma za kisheria, kama jamii itaelewa madhara ya ukatili, ukatili utakwisha na zaidi inapendeza sana kuona wasichana wameanza kujitambua, kujiamini na kupinga ukatili mbele ya hadhara". Amesisitiza Jan.
Naye Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, licha ya kulishukuru shirika hilo, ameitaka jamii kushirikiana kutokomeza ukatili wa kijinsia katika, jamii na kuwasisitiza viongozi wa mila na dini kushiriki katika mapambano hayo.
"Ninaamini viongozi wa dini na mila, wanaaminika sana ndani ya jamii, wakisimama na kupaza sauti kwa pamoja, mila potofu zitakwisha ndani ya jamii zetu, tunalo jukumu la kuhakikisha watoto wetu wanafikia malengo yao na kutimiza ndoto zao". Amesisitiza Mkurugenzi Msumi
Hata hivyo, watoto wa shule ya msingi Musa, wameweza kufikisha ujumbe kwa jamii kupitia nyimbo na mashairi, wakiwasisitiza wazazi na jamii kuachana na mila potofu za kuwakeketa na kuwaoza wasichana katika umri mdogo, kwani licha ya kukatiza ndoto zao lakini pia wanaathirika kisaikolojia, jambo ambalo linawatesa katika maisha yao yote.
Thomas Lunguya Mzee wa Mila, amesema kuwa jamii imeanza kuelewa juu ya madhara ya ukeketaji na ndoa za utotoni, na kuiomba Serikali kuendelea kutoa elimu kupitia majukwaa mbalimbali kwa kuwa wengi hufanya hivyo kutokana na uelewa mdogo.
"Ili ukatili wa kijinsia uweze kutokomea, bado inahitaji elimu ya kutosha kwa jamii, juu ya madhara ya ukeketaji na ndoa za utotoni kwa watoto wa kike, kwa kuwa wengi wakifahamu madhara yake, huamua kuachana na ndoa hizo" amesistiza mzee huyo wa mila.
Awali Mzee huyo wa mila, amelishukuru shirika la DSW na kuahidi kuendelea kushirikiana katika kupinga ukatili pamoja na kuendelea kuelimisha jamii kupambana na ukatili wa kijinsia katika eneo hilo.
Awali Shirika la DSW kwa kushirikiana na Serikali ya kijiji cha Olchoruvos, wamekarabati jengo la ofisi ya kijiji hicho na kupata eneo la Jengo la Binti salama, Ukumbi pamoja na ofisi za kijiji cha Olchoruvos na kata ya Musa kwa gharama ya shilingi milioni 12.8
Shirika hilo limekabidhi jengo hilo baada ya kulifanyia ukarabati, na kupata eneo la kutekelezea mradi wa Binti Salama, Ukumbi wa mikutano na sherehe, pamoja na ofisi za kijiji cha Olchoruvos na kata ya Musa.
ARUSHA DC
KaziInaendelea
JIANDAE KUHESABIWA
PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA MAKABIDHIANO YA KITUO
Mkurugenzi Mtendaji Halamshauri ya Arusha, Seleman Msumi, akishika alama ya Ufungu wa jengo la Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa, halmasahuri ya Arusha, jengo lililokabidhiwa na shirika la DSW Tanzania.
Mkurugenzi Mtendaji Halamshauri ya Arusha, Seleman Msumi, akikata utepe ikiwa ni ishara ya Ufunguzi wa jengo la Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa, halmasahuri ya Arusha, jengo lililokabidhiwa na shirika la DSW Tanzania.
Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la DSW Tanzania Jan Kreutzberg ( wa kwanza Kushoto) akizungumza na hadhara ya wananchi wa kijiji cha Olchoruvus kata ya Musa, kabla ya kukabidhi jengo la Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa
Mabinti wa kata ya Musa wakitumbuiza wakati wa uzinduzi wa jengo la Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa
Mabinti wa kata ya Musa wakifanya majadiliano ndani ya Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa, mara baada ya kituo hicho kuzinduliwa.
Mkurugenzi Mtendaji Halamshauri ya Arusha, Seleman Msumi, akizungumza na hadhara ya wananchi wa kijiji cha Olchoruvus kata ya Musa, kabla ya kukabidhi jengo la Kituo cha Mazingira Salama kwa Wasichana, katika kijiji cha Olchoruvos, kata ya Musa
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.