Na Elinipa Lupembe
Vijana halmashauri ya Arusha walionufaika na mikopo isiyo na riba inayotolewa na serikali, wameishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa na mkakati wa kuwawezesha vijana kupata mitaji na kuimarisha vipato.
Vijana hao wametoa kauli hiyo, wakati wa zoezi la kupokea mikopo iliyotolewa na halmashauri hiyo ikiwa ni asilimia 10 ya mapato yake ya ndani kwa robo ya pili ya mwaka wa fedha 2022/2023, hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya halmashauri hiyo.
Kwa umoja wao, vijana hao wameweka wazi kuwa mpango huwa wa serikali wa kuwapa mikopo isiyo na riba imewawezesha vijana kuongeza thamani kwenye kazi wanazozifanya na kujiingiza kwenye shughuli za ujasiriamali, shughuli zinazowaongezea kipato.
Habibu Malia kijana mwenye ulemavu, aliyekopeshwa shilingi milioni 10 na kununua bajaji, amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu kwa mpango huo wa kuwawezesha wananchi hasa vijana kujikwamua kiuchumi, mpango ambao unawainua vijana wengi hasa walioathirika na ukosefu wa ajira nchini.
Joseph Mibaroi wa kikundi cha KIDALI Youth Group cha kata ya Mwandeti, ameweka wazi kuwa awali alijishughulisha na kilimo na ufugaji wa nyumbani, lakini baada ya kupata elimu juu ya mikopo hiyo walijuinga kikundi na kukopeshwa milioni 10 fedha ambazo zimewatoa kwenye kilimo na ufugaji wa kawaida na kuwaingiza kwenye kilimo biashara kwa kununua mifugo na kuuza.
"Tunaishukuru serikali kwa kutupa mkopo wenye masharti nafuu, hata sisi vijana wa kijijini kabisa tumeweza kukopesheka, jambo ambalo halipatikani kwenye taasisi nyingine za kifedha, mkopo umetuinua na kuingai kwenye biashara sasa". Amesema Mibaroi
Naye Paulo Paskali amesema kuwa uchache wa vikundi vya vijana kujiingiza kwenye mikopo ni uoga na kushindwa kujiamini huku wengine wakidhani vikundi ni vya kinamaa, na kuiomba serikali kuendelea kuwajengewa uwezo wa kujiamini na namna bora ya kukopa, kwa kufanya hivyo vijana wanaweza kufanya mapinduzi ya kiuchumi kwenye jamii.
Aidha ameipongeza serikali, licha ya kutoa mikopo, watalamu wake wanafanya kazi kubwa sana ya kuelimisha na kuwaunganisha vijana ili wakidhi vigezo vya kupata mikopo hiyo, jambo ambalo linathamani na matokeo makubwa kwa vijana wa kitanzania, vijana ambao baadhi yao, ndoto zao zilikuwa zimeanza kufifia kwa kupoteza matumaini.
Hata hivyo vijana walikopeshwa wamewasihi vijana wote nchini kujitokeza kutumia fursa hiyo adhimu, ili waweze kujipatia mitaji ya kukuza pato la kijana mmoja mmoja, familia na jamii kwa ujumla wake.
Serikali kupitia halmashauri zote nchini inatoa mikopo isiyo na riba kwa kutoa 10 % ya mapato ya ndani kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi lengo likiwa ni kuwawezesha wananchi kiuchumi.
ARUSHA DC ni Yetu, Tushirikiane Kuijenga"
#KaziInaendelea✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.