Matumaini ya kupata nishati ya umeme yawashukia wananchi wa Mbuyuni kata ya Oljoro baada ya kusubiri nishati hiyo tangu kupatikana kwa Uhuru wa Tanganyika zaidi ya miaka hamsini iliyopita.
Matumaini hayo yakwenda mbali zaidi, baada ya Waziri mwenye dhamana kuagiza na kusisitiza nishati hiyo ya umeme uwafikie wananchi wote kwa kuzingatia kijiji kwa kijiji, kitongoji kwa kitongoji na hadi nyumba kwa nyumba.
Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema hayo alipotembelea na kukagua utekelezaji wa mradi wa umeme vijiji unaotekelezwa na Wakala wa Umeme Vijijini - REA katika eneo la Mbuyuni, halamshauri ya Arusha wilayani Arumeru.
Waziri Kalemani ameliagiza shirika la umeme TANESCO kupitia wakaka wa umeme vijijini-REA kuwaunganishia umeme wananchi wote bila kujali hadhi za nyumba zao wanazoishi.
Amesisitiza kuwa umeme uwekwe kwa mwananchi yoyote anaehitaji na mwenye uwezo wa kulipia gharama za kuunganisha hata kama nyumba yake ni ya udongo na kuezekwa kwa nyasi.
"Sitaki kusikia mneacha nyumba ya mtu kwa sababu hali duni ya nyumba, hali ya nyumba ya mtu haiwahusu" amesisitiza Waziri Kalemani.
Aidha amewataka wananchi hao kulipia gharama za kuunganishiwa umeme kiasi cha shilingi 27,000 tu na kuongeza kuwa endapo mtu atatozwa zaidi, atoe taarifa kwa viongozi wa ngazi ya wilaya na mkoa.
Hata hivyo Waziri huyo ameagiza umeme uunganishwe ndani ya siku saba baada ya mwananchi kukamilisha taratibu za malipo, na kuwataka wananchi kulinda miundombinu ya umeme katika maeneo yao na kujenga uzio kwenye transfoma.
Meneja wa TANESCO mkoa wa Arusha Gasper Msigwa amesema kuwa REA III kwa kipindi cha awamu ya kwanza itawaunganishia nishati ya umeme wateja wapatao 6,000 katika maeneo 58 ya mkoa wa Arusha, mradi utakao gharimu shilingi bilioni 9.3. Ameeleza kuwa hadi sasa jumla ya wateja 1,652 wamekamilisha taratibu za malipo na tayari miundombinu ya umeme imeksmilika kwa aslimia 90%.
Msigwa ameongeza kuwa, licha ya juhudi hizo za serikali ya awamu ya tano, bado shirika linakabiliwa na changamoto ya wizi wa nyaya za umeme na baadhi ya watu kukosa uaminifu na kujiunganishia umeme bila kufuata taratibu.
Loth Sabaya mkazi wa Oljoro amesema kuwa wamefurashwa na neema nishati ya umeme kijijini kwao, na kuongeza kuwa kukosa umeme kunawacheleweshea maendeleo,na wanashindwa kufanya shughuli za uzalishaji zinahitaji nishati ya umeme.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.