Na Elinipa Lupembe
Wasimamizi wa mradi wa ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule za sekondari, halmashauri ya Arusha, kupitia fedha za serikali shilingi milioni 760, maarufu kama 'Pochi la Mama', wametakiwa kutekeleza miradi hiyo kwa kuzingatia kanuni, sheria na taratibu za matumizi ya fedha za Umma.
Wasimamizi hao wamepata fursa hiyo, wakati wa kikao kazi maalum, chenye lengo la kukumbushana sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya matumizi ya fedha za Umma, katika utekelezaji wa miradi ya serikali, kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi amewataka wasimamizi hao, kushirikiana kwa pamoja kama timu katika utekelezaji wa mradi huo wa ujenzi vya vyumba vya madarasa na kuwasisitiza kufuata taratibu zote ikiwa ni pamoja na utunzaji wa taarifa zote muhimu na kukamilika kwa wakati ili kufikia lengonla kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza 2023.
"Fedha zimeshaingia kwenye akaunti za shule, tunakwenda kujenga vyumba 38 vya madarasa kwa milioni 20 kwa darasa likiwa na madawati 40, kupitia 'Force Akaunti' na kutumia ramani zilizotumika kwenye program ya EP4R, ndani ya siku 75, ujenzi uwe umekamilika, hakikisheni tunakamilisha kwa wakati". Ameagiza Mkurugenzi Msumi
Amefafanua kuwa Serikali imeweka taratibu za matumizi ya 'Force akaunti' ikiwa ni pamoja na ushiriki wa jamii katika ujenzi, hivyo ni wajibu wa kila mwenye dhamana ya kusimamia mradi kushiriki kutekeleza majukumu yake, lengo likiwa kuongeza uwazi na uwajibikaji wa jamii katika kusukuma gurudumu la maendeleo.
Naye Mkuu wa Idara ya Mipango, halmashauri ya Arusha, Anna Urio, amefafanua kuwa lengo la kikao hicho ni kukumbushana na kuwa na uelewa wa pamoja juu ya taratibu za matumizi ya fedha za Serikali katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa vyumba hivyo vya madarasa.
"Kila mwenye dhamana anatakiwa kufahamu kiasi cha fedha na idadi ya madarasa, muda wa utekelezaji, kuzingatia ubora wa mradi unaoendana na thamani ya fedha 'value for money', pamoja na ushirikishwaji wa jamii katika utekelezaji wa miradi kabla na wakati wote wa utekelezaji wa mradi". Amefafanua Afisa Mipango Anna.
Naye Mkuu wa Idara ya Ujenzi halmashauri ya Arusha, Mhandisi Nuru Mkwazu, ameahidi kuzingatia hatua za awali ikiwa pamoja na namna ya kupata wakandarasi na wazabuni kupitia ushindani kwa kuzingatia bei halisi ya soko na gharama za mradi pamoja na uteuzi wa kamati za usimamizi wa mradi.
Aidha kaimu Mweka Hazina, halmasahuri ya Arusha, Tido Moiro, amesisitiza kuhakikisha mkandarasi analipa kodi zote za Serikali, pamoja na asilimia 5 ya gharama ya mkataba 'retaintion', fedha ambayo itazuiliwa mpaka kazi itakapokamilika na endapo itatokea tatizo lolote pesa hiyo itatumika.
Hata hivyo walimu hao, wameupongeza uongozi wa halmashauri, kwa kikao kazi hicho ambacho wamekiri kina manufaa kwao, kutokana na ukweli kwamba, utekelezaji wa miradi hiyo unahitaji usimamizi imara wenye tija ili kufikia malengo ya serikali ya kuhakikisha wanafunzi wa kidato cha kwanza wanaingia darasani mapema Januari 2023.
Awali, kikao kazi hicho kimejumisha Maafisa Watendaji wa Kata, Maafisa Elimu kata na Wakuu wa shule zenye miradi, inayotekelezwa na fedha za pochi la mama.
ARUSHA DC
KaziIendelee
PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA KIKAO KAZI
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha Seleman Msumi, akizungumza na wasimamizi wa mradi wa ujenzi wa vyumba 38 vya madarasa, wakati wa kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
Afisa Mipango, halmashauri ya Arusha Anna Urio, akitoa maelekezo ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa vyumba 38 vya madarasa, wakati wa kikao kazi na wasimamizi wa mradi, kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
Mkuu wa shule sekondari Einot, Mwl. Swai akibadilishana uzoefu wa changamoto na utatuzi aliyokutana nayo wakati wa utekelezaji wa ujenzi wa madarasa ya UVIKO 19, wakati wa kikao kazi cha wasimamizi wa mradi wa ujenzi wa madarasa ya Pochi La Mama, kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri
Baadhi ya wasimamizi wa ujenzi wa vyumba vya madarsa 38, wakifuatilia, maelekezo, mijadala na maoni ya utekelezaji wa mradi huo wakati wa kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.