Na. Elinipa Lupembe.
Katika kukabiliana na upungufu wa vyumba vya madarasa unaozikabili shule nyingi nchini, unaosababishwa na ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa shuleni, katika awamu hii ya tano, kutokana na Serikali kutekeleza elimu bila malipo.
Halmashauri ya Arusha imeendelea kutekeleza miradi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule zake, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo, wa ndani na nje ya nchi, ili kukabiliana na upungufu huo.
Shule ya sekondari ya Sokon II kata ya Sokon II, ni miongoni mwa shule za Sekondari, Halmashauri ya Arusha, ambayo imepata neema ya pekee ya kujengewa vyumba vinne vya madarasa na vyoo, kwa ufadhili wa Ubalozi wa Japani nchini Tanzania.
Mkurugenzi Mtendaji, Halmashauri ya Arusha Dkt. Wilson Mahera ameeleza kuwa, ubalozi wa Japani umetoa kiasi cha shilingi milioni 196.2, kwa ajili ya kukamilisha, ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa, vyoo vya wanafunzi, pamoja na samani za madarasa hayo pindi ujenzi huo utakapokamilika.
Aidha, Dkt. Mahera amefafanua kuwa, kiasi hicho cha fedha kitatumika, kujenga msingi wa jengo la ghorofa la sakafu tatu, na kukamilisha vyumba hivyo vinne vya madarasa, huku kila sakafu ikitarajiwa kuwa na vyumba vinne na vyoo vya wanafunzi, na kufanya jengo hilo lote, kuwa na jumla ya vyumba 12 pindi litakapokamilika.
"Kutokana na uhaba wa ardhi, jengo hilo litakuwa la ghorofa, na kiasi hicho cha fedha, kitatumika kujenga msingi wa ghorofa hilo, na kukamilisha vyumba vinne vya madarasa na vyoo vya wanafunzi pamoja na meza na viti vya wanafunzi" amethibitisha mkurugenzi Mahera
Naye Mkuu wa shule ya Sekondari Sokon II,mwalimu Mwamvita Kilonzo, amesema kuwa, kukamilika kwa vyumba hivyo vya madarasa, kutapunguza msongamano wa wanafunzi darasani kwa asilimia 36% kutoka upungufu wa vyumba 11 vya madarasa uliokuwepo.
Ameongeza kuwa, Vyumba hivyo vya madarasa vinategemewa kusomea jumla ya wanafunzi 189 kwa uwiano wa wanafunzi 45 kwa darasa moja, na kutasaidia kuwa na mazingira rafiki kwa walimu na wanafunzi ya kuwezesha kitendo cha kufundisha na kujifunza kuwa rahisi.
Awali, Shule ya sekondari Sokon II ina jumla ya Wanafunzi 1,013, kutokana na idadi hiyo ya wanafunzi, shule hiyo ilikuwa na upungufu wa vyumba 11 vya madarasa, na baada ya kukamilika vyumba hivyo 4, kutakuwa na upungufu wa vyumba 7 ambayo tayari kuna mikakati ya ujenzi wa vyumba hivyo.
Halmashauri ya Arusha inatekeleza kwa vitendo, mikakati na Sera za serikali ya awamu ya tano, inayoongozwa na mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliyoahidi watanzania kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, wakati wa Uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.