Na. Elinipa Lupembe
Halmashauri ya Arusha imemaliza mwaka wa fedha 2017/18 na kuanza mwaka mpya wa fedha 2018/19, kwa neema kubwa ya kupata miradi mitatu yenye thamani ya shilingi milioni 780.
Akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake, Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha Dkt. Wilson Mahera, amethibitisha kuwa, halmashauri yake, imepokea fedha kiasi cha shilingi milioni 780 kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa mitatu ikiwa miradi miwili ya elimu na mradi mmoja wa afya.
Dkt. Mahera ameitaja miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa bweni na vyumba vinne vya madarasa, shule ya sekondari Mringa kwa gharama ya shilingi milioni 230.
Kiasi cha shilingi milioni 150, kitatumika kujenga vyumba vya madarasa, ofisi ya walimu pamoja na vyoo, kwa ajili ya kuanzisha shule, mpya ya sekondari Kiseriani katika kata ya Mlangarini.
Ameongeza kuwa, fedha nyingine kiasi cha shilingi milioni 400, zimepokelewa kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na upanuzi wa kituo cha Afya Mbuyuni kata ya Oljoro.
Aidha Dkt. Mahera, amefafanua kuwa fedha hizo zimetokana na vyanzo mbalimbali vya fedha hizo, kiasi cha shilingi milioni 230 ni fedha ikiwemo fedha za mradi wa Lipa Kutokana na Matokeo 'P4R', milioni 400 fedha za serikali za kuendeleza vituo vya Afya nchini, huku shilingi milioni 230 zikiwa ni fedha za fidia ya shamba la kijiji lililotolewa kwa chuo kikuu Mzumbe.
Hata hivyo Mkurugenzi Mahera amesema kuwa, miradi hiyo itaanza kutekelezwa mara baada ya kufanya mikutano ya wananchi wa maeneo ambayo miradi hiyo itatekelezwa.
Aidha Mkurugenzi huyo amesema kuwa, lengo la kukutana na wananchi ni kuwashirikisha juu ya ushiriki wao katika utekelezaji wa miradi hiyo, kwa kuwa miradi yote itatumia Force Account ambayo inaruhusu miradi hiyo kutumia mafundi wa eneo husika 'local fundi' chini ya usimamizi wa wananchi.
Mkurugenzi huyo amewataka wananchi wa maeneo hayo kushiriki kwa hali na mali katika utekelezaji wa miradi hiyo huku akiwataka wadau mbalimbali kujitokeza kuongeza nguvu katika ujenzi wa miradi hiyo.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.