HALMASHAURI YA WILAYA YA ARUSHA YAZINDUA MASHINDANO YA UMISSETA NGAZI YA WILAYA ILI KUPATA TIMU ZA KUSHIRIKI NGAZI YA MKOA
Katika juhudi za kuibua na kukuza vipaji vya michezo kwa vijana wa shule za sekondari, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha imezindua rasmi mashindano ya Umoja wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) yaliyofanyika leo 09 Mei, 2025 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Ilboru.
Uzinduzi huo ulifanywa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha ambaye pia ni Afisa Elimu Sekondari na mlezi wa michezo wa Halmashauri hiyo, Menard Lupenza, ambapo alisisitiza kuwa mashindano hayo ni jukwaa muhimu la kuwapata wachezaji bora wapatao 120 watakaoiwakilisha Halmashauri hiyo katika ngazi ya Mkoa.
"Mashindano haya yamepitia hatua mbalimbali kuanzia ngazi ya shule hadi kata, na sasa tunashuhudia hatua ya Wilaya ambayo itatupatia kikosi cha Halmashauri ya Arusha kitakachoshiriki UMISSETA 2025 kwenye mashindano ya kimkoa," alisema Lupenza.
Aliainisha michezo inayoshindaniwa kuwa ni riadha, mpira wa miguu, mpira wa pete, mpira wa kikapu na kurusha mkuki.
Kwa upande wake, Afisa Michezo wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, Priscus Silayo, alibainisha kuwa mashindano hayo yanajumuisha kanda nne za Halmashauri hiyo ambazo ni: Mlangarini, Kisongo, Ilboru na Ngaramtoni.
Lupenza pia alitumia fursa hiyo kuwapongeza walimu wa michezo, wataalamu, na wote waliowezesha vijana kufika hatua hiyo muhimu. Alisisitiza kuwa michezo si burudani tu, bali ni njia muhimu ya kuwaepusha watoto na vishawishi mbalimbali vinavyowakumba katika jamii ya sasa.
"Vijana wetu wapo tayari kushindana. Wameiva kisawasawa, na tunatarajia timu imara itakayoleta heshima kwa Halmashauri yetu katika mashindano ya mkoa," aliongeza.
Viongozi wote wa Halmashauri, waalimu, wakufunzi, wanafunzi na wanamichezo walionyesha mshikamano mkubwa na ari ya juu ya kushiriki, hali iliyotia matumaini makubwa kwa mustakabali wa michezo wilayani humo.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.