Na. Elinipa Lupembe
Jamii imehimizwa kujipangia kutoa msaada wa kimwaili na kijamiii kwa familia zenye uhitaji kuweza kurejesha Faraja na matumaini kwao ikiwa ni pamoja na kuwasaidia watoto wanaotokea katika familia hizo kukua katika malezi bora na hatimaye kutimiza ndoto zao.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Arusha Seleman Msumi, wakati akikabidhi msaada wa chakula kwa familia tisa zenye uhitaji, ikiwa ni zawadi maalum ya sikukuu ya mwaka mpya 2023, washerehekee kwa furaha na amani kama familia zingine.
“Sisi kama halmashauri, tumeguswa na hali za hawa wananchi wetu, tumeona ni vyema kutoa msaada wa chakula ili ndugu zetu waweze kuungana na watanzania wengine kusherekea sikukuu za mwisho wa mwaka huu.” Amesema Mkurugenzi Msumi.
Kwa upande wake Afisa Ustawi wa Jamii Halmashauri ya Arusha, Beatrice Tengi, licha ya kuzishukuru familia hizo, ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wadau wengine kujitokeza kwa wingi na kutoa misaada ya namna hiyo ili iweze kuzifikia familia nyingine zenye uhitaji.
Hata hivyo familia hizo zimeishukuru sana halmashauri kwa kuendelea kuwakumbuka wananchi wake kwani inaonesha jinsi serikali inavyowapenda na kuwajali wananchi wake hasa wenye mahitaji maalumu kwa kuwapa misaada mbalimbali.
Akizungumza kwa niaba ya familia hizo zilizopokea msaada huo wa chakula, Maria Nicolaus, mkazi wa Sanawari, amesema anaitakia mema Serikali ili iendelee na moyo huo wa upendo wa kuwajali watu wenye mahitaji maalum kwani inawapa Faraja na matumaini ya kuishi.
Aidha, msaada huo uliotolewa ni pamoja na mchele kg. 150, sabuni miche 25, sukari kg. 25, unga wa ugali kg.25, unga wa ngano kg. 50, mafuta lita 30, maharage kg.20, katoni 5 za juice, chumvi, majani ya chai, sabuni za unga pamoja na taulo za kike pcs 24 ukiwa na thamani ya shilingi milioni 1.14.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.