Na Elinipa Lupembe.
Watalamu halmashauri ya Arusha, wameagizwa kuendelea kuikumbusha Serikali, kupata vibali vya kuajiri watumishi, kutokana na upungufu wa watumishi katika sekta ya elimu, afya na utawala, upungufu ambao unakwamisha upatikanaji wa huduma stahiki kwa wananchi.
Rai hiyo imetolewa na wajumbe wa Baraza la waheshimiwa madiwani, kwenye mkutano wa baraza la Madiwani la kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa shughuli za kata kwa kipindi cha kuanzia mwezi Oktoba mpaka Desemba 2021, mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
Licha ya wajumbe hao, kuwasilisha mafanikio, maendeleo na mipango ya kata zao, waliweka wazi changamoto ya upungufu wa watumishi katika maeneo yao, changamoto inayokwamisha upatikanaji wa baadhi ya huduma kwa wananchi, ikiwemo maafisa watendaji wa vijiji, watumishi wa afya katika zahanati na vituo vya afya, pamoja na walimu hasa kata za pembezoni.
Wajumbe hao wameongeza kuwa, serikali kwa kushirikiana na wananchi wamejitahidi sana kuchangia ujenzi wa miundo mbindu ya zahanati, ofisi za vijiji pamoja na vyumba vya madarasa, changamoto inayojitokeza sasa ni upungufu wa watumishi wa kutoa huduma kupitia majengo yaliyojengwa kwa gharama kubwa.
"Tumejenga zahanati, nyingine zimefunguliwa na nyingine yapo majengo tu, lakini hakuna daktari wala wauguzi, ofisi nyingi za vijiji hazina watendaji wa vijiji, tunawaomba watalamu wetu, endeleeni kuisumbua serikali yetu makini, kuajiri watalamu katika maeneo hayo, ili wananchi wetu wapate huduma, kukosekana kwa watalamu kunawavunja moyo wananchi wanaojitolea kujenga miundo mbinu ya kupatia huduma katika maeneo yao" wamesisitiza wajumbe hao.
Aidha Waheshimiwa Madiwani wa kata za Nduruma, Bangata, Oldonyowas, Kiosongo na Musa wamelalamikia ukosefu wa watumishi wa afya kwenye zahanati ambazo tayari zimekamilika ujenzi katika maeneo yao.
Naye Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya Arusha, Mheshimiwa Feddy Mollel, amehitimisha mkutano huo kwa kumuagiza mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, kuendelea kuwasilisha idadi ya upungufu wa watumishi katika sekta ya afya, idadi ya maafisa watendaji wa vijiji ili serikali iweze kutoa kibali cha kuajiri watumishi hao na kusisitiza kuzisajili zahanati zote ambazo zimekamilika lakini bado hazijapata kusajiliwa.
"Inasikitisha sana, wananchi kwa sasa wana mwamko wa kujiletea maendeleo yao wenyewe, wamejitahidi kujenga miundo mbinu ya zahanati, na kukamilisha, lakini baadhi ya zahanati hazifanyi kazi, kutokana na kukosa watalamu, hii inawakatisha tamaa wananchi wetu, tuiombe serikali yetu sikivu ifanye jambo" amesisitiza Makamu Mwenyekiti huyo.
Akijibu maswali yaliyoulizwa na waheshimiwa madiwani, kuhusu ukosefu wa watumishi katika zahanati na ofisi za vijiji, Afisa Rasilimali watu Halmashauri ya Arusha, Elizabeth Ngobei, amefafanua kuwa, halmashauri tayari imeomba kibali cha kuajiri Maafisa Watendaji 11 wa vijiji, huku idadi ya upungufu wa watumishi katika sekta ya Afya, ikiwa imewasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI, kinachosubiriwa ni kibali cha ajira kutoka serikali Kuu.
Aidha Afisa Rasilimali watu huyo, ameweka wazi kuwa, licha ya changamoto ya upungufu wa watumishi katika maeneo hayo, serikali inatoa miongozo ya kuwatumia watumishi waliopo, kuhakikisha wananchi wanapata huduma katika maneo yasiyo na watumishi.
"Tunatambua upungufu wa watumishi kisekta, tumeomba kibali cha kuajiri Maafisa Watedaji 11 wa vijiji, tunasubiri kibali cha ajira kutoka Serikali Kuu, lakini Serikali inatoa miongozo ya kuwatumia watumishi waliopo ili kazi zisikwame na wananchi waendelee kupata huduma licha ya changamoto zilizopo" amesema Elizabeth
Hata hivyo Kaimu Mkurugenzi halmashauri ya Arusha, Paulus Kessy, amekiri kupokea maelekezo hayo na kuahidi kuendelea kufuatilia upatikanaji wa vibali vya ajira kwa watumsihi hasa katika zahanati na ofisi za vijiji, maeneo ambayo yanaonekana kupwaya katika upatinaji huduma kwa wananchi, licha ya kuwa suala la upufungufu wa watumishi si la halmashauri ya Arusha pekee bali ni changamoto ya nchi nzima.
Awali katika mkutano huo wa Baraza la Madiwani wa kuwasilisha taarifa za kata, kwa kipindi cha robo ya pili kwa mwaka wa fedha 2021/22, waheshimwa madiwani wa kata zote 27, wameipongeza na kuwa na imani kubwa na Serikali yao ya awamu ya sita, kwa kupelekea fedha nyingi za miradi ya maendeleo katika maeneo yao, na kuiomba serikali kuendelea kutatua changamoto ndogo ndogo zinazojitokeza katika maeneo yao.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.