Na Mwandishi wetu
Baada ya Serikali kutoa fedha hivi karibuni kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule za sekondari Nchini, waheshimiwa madiwani halmashauri ya Arusha wameiomba Serikali sasa kutupia macho katika upande wa shule za Msingi kwa kuanza utekelezaji wa ukarabati wa miundombinu chakavu hasa katika shule kongwe Pamoja na ujenzi wa vyumba vya madarasa na vyoo katika baadhi ya shule hizo.
Hayo yamejiri wakati wa Kikao cha Waheshimiwa Madiwani cha kujadili taarifa za utekelezaji wa shughuli za maendeleo za Kata kwa robo ya kwanza ya mwaka wa Fedha 2022/2023 kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa halmashauri hiyo.
Wakiwasilisha taarifa za utekelezaji wa Kata, Waheshimiwa Madiwani wamewasilisha changamoto kubwa ya uchakavu wa miundombinu ya shuoe za msingi wamesema kuwa kuna uhitaji mkubwa wa ukarabati na ujenzi wa miundombinu katika shule za msingi, miundombinu ambayo ilijengwa miaka mingi iliyopita na kujenga hofu inayohatarisha usalama wa wanafunzi wenaosoma katika shule hizo.
Diwani wa kata ya Bangata Mhe. Ezra Tomito, amezitaja baadhi ya changamoto zinazokabili miundombinu ya shule za misngi ni pamoja na baadhi ya vyumba vya madarasa kuwa na sakafu ya udongo, uchakavu wa milango na madirisha, kuta na mapaa, uchakavu unaotokana na kujengwa na kutumika miaka mingi iliyopita hali inayopelekea wanafunzi katika shule hizo kuwa na wasiwasi kuhusu usalama wao.
"Baadhi ya shule zetu za Msingi zina ubovu wa miundombinu ambayo inahitaji ukarabati wa haraka kwa mfano, Shule ya Msingi Seliani yenye miaka zaidi ya mia moja (100) ni moja ya shule inayohitaji ukukarabati wa miundombinu yake karibu yote”. Alisema Mhe. Eliakimu Marivey,
Diwani Kata ya Kimnyaki.Diwani wa kata ya Sokon II, Mhe. Obed Mollel, ameiomba na kuishauri Serikali kuanza kutenga fungu la fedha kwa ajili ya kukarabati miundombinu ya shule za msingi kama inavyofanyika kwa shule za sekondari, ili wanafunzi waweze wapate masomo kwenye mazingira salama.
Akitolea ufafanuzi changamoto hiyo, Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Arusha Seleman Msumi, amesema kuwa Serikali imejipanga vizuri kwa ajili ya kutatua changamoto za miundombinu ya shule za msingi na hivi karibuni utakelezaji wa ukarabati wa miundombinu iliyochakaa pamoja na ujenzi wa vyumba vipya vya madarasa kwa shule zenye uhitaji utaanza ili wanafunzi wanaosoma katika shule hizo wasome kwa amani.
“Serikali inafahamu changamoto iliyopo katika miundombinu ya shule za Msingi hasa zile kongwe, na sasa kuna Mradi wa BOOST unaendelea kufanya tathmini ya uchakavu wa miundombinu kwa shule hizo, mara baada ya kukamilika kwake utatuzi wa changamoto hiyo katika shule za Msingi zenye uchakavu na uhaba wa vyumba vya madarasa utaanza kufanyiwa kazi”. Alisema Mkurugenzi Msumi.
Sambamba na hayo, Mkurugenzi Msumi amesema kuwa serikali imejipanga kwa mwaka huu wa fedha kutekeleza miradi mbalimbali kisekta ikiwemo Sekta ya Afya katika hospitali ya Wilaya ya Oltrumet kwa kujenga Uzio pamoja na mahitaji mengine ya maabara, jingo la Mionzi pamoja jingo la Mochwari.
Awali Mkutano wa wazi wa Baraza la Madiwani umefanyika kwa mujibu wa sheria na kanuni za serikali za mitaa ukiwa na ajenda sita (6) huku ajenda kuu ikiwa ni kuwasilisha taarifa za utakelezaji wa shughuli za maendeleo za kata zilizofanyika kwa ipindi cha miezi mitatu.
PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA MKUTANO WA BARAZA
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.