Na Elinipa Lupembe
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Deogratius John Ndejembi ameuagiza uongozi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), kutekeleza ujenzi wa uzio katika shule ya sekondari Oldonyowas ili kulinda Miundombinu ya madarasa na mabweni iliyojengwa katika shule, ikiwa ni pamoja na usalama wa wanafunzi wa shule hiyo.
Naibu Waziri Ndejembi amesema hayo wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa ujenzi wa mabweni mawili ya wavulana katika shule hiyo, Mradi unaotekelezwa na TASAF III awamu ya II kwa ufadhili wa OPEC International Fund, na kuweka wazi kuwa, kukamilika kwa miundombinu ya shule hiyo, uende sambamba na ujenzi wa uzio wa shule hiyo ili kuhakikisha usalama wa shule na wanafaunzi.
“Nimeridhishwa na maendeleo ya ujenzi huu wa mabweni kutokana na ushirikishwaji wa wananchi wa eneo hili, kwa kuwapa ajira za muda na kujipatia kipato kama ilivyo mpango wa TASAF wa kuzikomboa kaya zenye kipato cha chini, niwatake TASAF kuweka mkakati wa kujenga uzio katika shule hii kwa ajili ya usalama wa mali na wanafunzi”. Amesema Mhe. Ndejembi
Naye Mbunge wa jimbo la Arumeru Magharibi Mhe. Noah Lembris amesema kuwa uwepo wa mabweni hayo utasaidia utulivu kwa wanafunzi hasa wale wanaotembea umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni kuondokana na adha hiyo, hali itakayochangia kupanda kwa taaluma na ongezeko la ufaulu kwa wanafunzi shuleni hapo.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhandisi Richard Ruyango, licha ya kuishukuru serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni hayo, amewataka viongozi pamoja na wananchi kila mtu kutekeleza wajibu wake kama kanuni na taratibu za serikali zinavyoelekeza ikiwemo kutunza na kulinda miradi yote inayotekelezwa na Serikali katika maeneo yao.
Awali akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Oscar Maduhu, amesema kuwa lengo la miradi hiyo ni kuondoa adha iliyopo katika maeneo yenye uhaba wa miundombinu katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya elimu na afya, lengo likiwa ni kupambana na adui maradhi, ujinga na umasikini.
“TASAF itaendelea kutekeleza miradi mingine kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kisekta, niwatake wananchi kuendelea kujitoa katika kutekeleza miradi pamoja na kuhakikisha miradi hiyo, inakamilika kwa viwango vinavyokubalika, ili kufikia lengo la serikali la kuwahudumia wananchi wa kipato cha chini, zaidi niwatake kuitunza miradi hiyo ili idumu kwa muda mrefu na kuhudumia wanafunzi wetu”. Amesisitiza Maduhu.
Elieshi Gabriel ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Oldonyowas ameweka wazi kuwa, Watoto wao walikuwa wanatembea umbali mrefu sana wakivuka makorongo makubwa kufika shuleni hapo, na wakifika nyumbani wanakuwa wamechoka sana kiasi cha kutoweza kujisomea wenyewe hivyo uwepo wa mabweni hayo utasadia Watoto wao kuwa salama na ufaulu wao kuongezeka.
Mradi huo wa ujenzi wa mbweni mawili ya wavulana umetekelezwa kwa gharama ya Zaidi ya shilingi milioni 300 baada ya kukamilika kwa mabweni ya wasichana katika shule hiyo na yanatarajiwa kubeba jumla ya wanafunzi 160.
ARUSHA DC
KaziInaendelea
JIANDAE KUHESABIWA.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Deogratius John Ndejembi, akikagua mradi wa ujenzi wa Mabweni ya wavulana shule ya sekondari Oldonyowas, mradi unaotekelzwa na TASAF kwa gharama ya shilingi milioni 300.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Deogratius John Ndejembi, akikagua mradi wa ujenzi wa Mabweni ya wavulana shule ya sekondari Oldonyowas, mradi unaotekelzwa na TASAF kwa gharama ya shilingi milioni 160.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.