Na. Elinipa Lupembe.
Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mheshimiwa John Mongela amewaongoza wafanyakazi wote wa mkoa wa Arusha, kwenye maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Mei Mosi, 2022, maadhimisho yaliyofanyika kwenye viwanja vya General Tyre eneo la Njiro, Jijini Arusha.
Mkuu huyo wa mkoa amewapongeza wafanyakazi wote kwa siku hiyo muhimu Duniani, huku akiweka wazi kuwa Serikali inatambua na kuthamini kazi kubwa inayofanywa na wafanyakazi wote wa nchini, kazi ambayo ndio msingi wa maendeleo ya Taifa la Tanzania.
"Ninawapongeza sana wafanyakazi wote wa mkoa wa Arusha katika sekta zote, kwa kazi kubwa tunayofanya, kwa maendeleo ya mkoa wetu na taifa kwa ujumla, nawapongeza sana waajiri wote wa Mashirika na Taasisi binafsi, kwa mchango mkubwa wenye tija kwa mkoa na taifa lote kwa ujumla". Amesisistiza Mkuu huyo wa mkoa
Aidha Mheshimiwa Mongela, ameongeza kuwa, usalama wa mkoa wa Arusha, unachangiwa kwa kiasi kikubwa na wafanyakazi, kutokana na watu kuelekeza nguvu, akili na mawazo yote kwenye kufanya kazi, na kuwasisitiza wafanyakazi wote kuendelea kuwa na mshikamano, katika sekta zote, jambo ambalo kimsingi ndilo lenye kuleta tija kwa maendeleo ya Taifa.
Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa, amewataka waajiri wote, kuwatambua na kuwapa zawadi stahiki kwa wafanya kazi hodari kila mwaka, jambo ambalo linaongeza motisha kwa wafanyakazi, kuendelea kufanya kazi kwa bidii, pamoja na kupiga marufuku tabia ya baadhi ya waajiri kushindwa kuwatambua wafanyakazi hodari, na baadhi kuwatambua na kutokuwapa zawadi zao stahiki.
Maadhimisho hayo, yalipambwa na mabango yenye jumbe mbalimbali, ndelemo na vifijo wakati wa maandamano wafanyayakazi hao, pamoja na maonesho ya kazi za taasisi na mashirika mbalimbali zikipita mbele ya mgeni rasmi ndani ya magari.
Awali maadhimisho hayo kwa mwaka 2022, yenye Kauli Mbiu ya "Mishahara na Maslahi Bora kwa Wafanyakazi Ndiyo Kilio Chetu", Kazi iendee, ikionesha namna wafanyakazi wana ari ya kufanya kazi inayokwenda sambamba na mishahara na maslahi bora kwa wafanyakazi wa sekta zote.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.