Na Elinipa Lupembe
Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluh Hassan imewahakikishia wanafunzi 7,856 walifaulu mtihani wa darasa la saba mwaka 2022 sawa na asilimia 100, wamepangiwa shule za sekondari za serikali halmashauri ya Arusha
Uthibitisho huo umetolewa na Mkuu wa wilaya ya Arumeru, Mhandisi Richard Ruyango wakati wa hafla ya makabidhiano ya mradi wa ujenzi wa vymba 38 vya madarasa, vilivyojengwa maalum kwa ajili ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza Januari 2023.
Mkuu huyo wa wilaya amesema kuwa, kutokana na uwepo wa vyumba vya madarasa 134, ambavyo serikali imewekeza kwa miaka miwili mfululizo vitawezesha idadi hiyo ya wanafunzi kuanza masomo yao mapema Januari 9.
"Mwishoni mwa mwaka 2021 tulipokea shilingi bilioni 2 na kujenga vyumba 96 vya madarasa na mwaka huu tumepokea milioni 769 na kujenga vyumba 38 kwenye shule 18 zilizokuwa na upungufu, madarasa hayo yatatumika kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha kwanza 2023". Ameweka wazi Mhandisi Ruyango.
Hata hivyo amewataka viongozi wote kusimamia na kuhakikisha wanafunzi wote waliopangiwa kujiunga na elimu hiyo ya sekondari, wanaanza masomo ifikapo tarehe 9 Januri 2023 na kuwaasa wazazi kuwapatia mahitaji yao ya msingi ya shule kama ilivyo kwenye fomu za kujiunga na shule hizo.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Arusha, Mhe. Ojungu Salekwa amethibitisha kuwa, serikali imeshafanya kazi yake, kazi iliyobaki ni kuhakikisha wanafunzi wote waliopangiwa kujiunga na kidato cha kwanza wanakwenda shule kwa wakati na kwa idadi kamili ya wanafunzi waliochaguliwa.
"Mama Samia ameshafanya kazi yake, kazi yetu ni moja kuhakikisha wanafunzi wote waliopangiwa kujiunga na kidato cha kwanza wanaanza shule kwa wakati, na wazazi kuhakikisha wanawapa watoto wao mahitaji yote ya shule". Amesema Mhe. Ojung'u
Joshua Augustino mwanafunzi anayeingia Kidato cha pili shule ya sekondari Mringa licha ya kuishukuru Serikali kwa kuwajengea nmadarasa mazuri, ameahidi kusoma kwa bidii ili kufikia malengo yake na kuja kulitumikia Taifa lake la Tanzania.
Mwenyekiti wa Bodi ya shule ya sekondari Mringa Mwl. Jackson Mollel amesema kazi iliyofanywa na serikali ni kubwa na inathamani kwa watoto na vizazi vyao, kazi ambayo imewapunguzia wananchi mzigo wa kuchangia ujenzi wa madarasa, michango ambayo ilikiwa inasuasua na kushindwa hata kukamilisha darasa moja kwa wakati.
Akiwasilisha taarifa ya mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji halmasahuri ya Arusha, Seleman Msumi, amesema kuwa halmashauri ilipokea shilingi milioni 760 na kujenga vyumba 38 vya madarasa, viti na meza 50 kwa kila darasa pamoja na ofisi 7 za walimu kwenye shule 6 kati ya shule, kwenye shule 18 za sekondari.
Ifahamike kuwa ujenzi wa vyumba vya madarasa ni utelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 79 kifungu (q) Kukarabati miundombinu ya kufundishia na kujifunzia katika shule za Msingi na Sekondari nchini.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.