Na. Elinipa Lupembe.
Shirika La Girls LiveliHood & Mentorship Initiative 'GLAMI', limekamilisha na kukabidhi mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Arusha, mradi wa ujenzi wa miundo mbinu ya choo cha wasichana chenye matundu 10, mradi uliogharimu shilingi milioni 22.2 kwa shule ya sekondari Mringa.
Akikabidhi mradi huo, Mkurugenzi wa Miradi shirika la GLAMI, Asimwe Sued, amesema kuwa, shirika hilo, limejenga miundo mbinu hiyo ya choo cha kisasa, lengo likiwa kuwasaidia na kuwawezesha wasichana kusoma kwa amani na utulivu, hasa kwa kuzingatia changamoto za kiafya na kimazingira zinazoathiri wasichana kwenye masomo yao, wakati wakiwa kwenye hedhi.
Ameongeza kuwa, wasichana wanapata changamoto kubwa wakati wa hedhi wawapo shuleni, kwa kukosa sehemu za kujisitiri kutokana na shule nyingi kukosa miundo mbinu hiyo, hivyo shirika limeona ni vyema kuungana na serikali kwa kujenga miundo mbinu ya choo, yenye sehemu ya kubadilishia taulo wakati wakiwa kwenye hedhi.
"Shirika limezingatia, Hedhi Salama kwa watoto wa kike wawapo shuleni, lengo ni kuwawezesha wasome kwa amani na kuhudhuria masomo yao, bila kukosa vipindi kwa sababu ya hedhi na zaidi waweze kufikia malengo na kutimiza ndoto zao" amesema Mkurugenzi Asimwe.
Hata hivyo Mkurugenzi Asimwe, ameweka wazi miradi inayotekelezwa na shirika hilo katika halmashauri ya Arusha, miradi miwili ya KISA na BINTI SHUPAVU na kufafanua kuwa mradi wa KISA, unaotoa mafunzo ya uongozi na stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike wa kidato cha tano na cha sita huku mradi wa BINTI SHUPAVU, ukitoa mafunzo ya uongozi binafsi na stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike wa kidato cha kwanza hadi cha nne.
Naye Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, amepokea mradi huo kwa kuwashukuru wadau hao wa maendeleo wa shirika la GLAMI, kwa msaada huo, na kuthibitisha kuwa uwepo wa miundo mbinu ya choo cha kisasa chenye sehemu ya kujistiri wasichana wakati wa hedhi, licha ya kuhakikisha afya za watoto hao, lakini itaongeza mahudhurio kwa wasichana na kupandisha taaluma kwa wasichana hao.
"Tunafahamu wasichana wengi hukosa masomo, kipindi cha hedhi, takwimu zinaonyesha, mtoto wa kike hushindwa kuhudhuria vipindi 3-4 kwa mwezi, vipindi 48 kwa mwaka wakati wa hedhi, uwepo wa miundo mbinu hii, utaongeza siku za msichana kuhuduria masomo bila kukosa, niwasihi kuvitunza vyoo hivi kwa kuwa, wafadhili wametumia fedha nyingi, kujenga" ameweka wazi Mkurugenzi Msumi
Naye mkuu wa shule sekondari Mringa, Mwalimu Salim Magaka, licha ya kulishukuru shirika hilo kwa kujenga miundombinu ya vyoo vya wasichana shuleni hapo, amesema kuwa, miundo mbinu hiyo imejengwa wakati muafaka kutokana na ukweli kwamba, shule ilikuwa inakabiliwa na upungufu wa matundu ya vyoo, hasa ulinganisha na idadi kubwa ya wanafunzi shuleni hapo, choo hicho kitakuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi hasa wa kike.
Aidha amepongeza pia uwepo wa choo cha kisasa chenye miundo mbinu ya kujisitiri watoto wa kike jambo ambalo, ilikuwa ni changamoto kubwa shuleni hapo, na kuongeza kuwa, anaamini changmoto ya wasichana kushindwa kuhudhuria masomo wakati wa hedhi itapungua kwa kiasi kikubwa.
Awali halmashauri ya Arusha kwa kushirikiana na shirika la GLAMI linatekeleza miradi yake ya Kisa na Binti Shupavu kwenye shule 10 za sekondari za Mringa, Mwandet, Mlangarini, Enaboishu na Cornerstone, pamoja na mradi wa Kisa kwenye shule za sekondari Mukulat, Einoth,Kimnyaki, Mateves, Mwandet na Ilkidin'ga.
ARUSHA DC
KaziInaendeleaaa...✍✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.