Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi maalum Dkt.Doroth Gwajima, ameitaka Jamii na wadau mbalimbali kuungana kwa pamoja katika vita dhidi ya vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto. Rai hiyo ameitoa katika maadhimisho ya siku ya mwanamke anayeishi kijijini, ambapo kitaifa yamefanyika Oktoba 15, 2023 katika kijiji cha Olevolos kata ya Kimyaki Halmashauri ya Arusha wilayani Arumeru.
Dkt.Gwajima amesema kuwa, hali ya vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto nchini bado viko juu na kwamba lazima jamii ibadilike kimtazamo, kwani takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kwa kipindi cha mwaka mmoja jumla matukio 12,000 ya watoto wamefanyiwa vitendo vya ukatili, kati ya idadi hiyo watoto 10,000 walikuwa ni wa kike na kati ya hao watoto 6,000 walikumbwa na ukatili ya kingono.
Amesema kutokana na kushamiri kwa matukio hayo, Wizara yake kushirikiana na wadau mbalimbali wanaoshughulikia masuala ya kupinga ukatili kwa wanawake na Watoto, wataendelea kutoa elimu kwa Jamii ili kuweka nguvu ya pamoja kukabiliana na janga hilo kwa kuwabaini wahusika na kuwafikisha katika vyombo vya sheria ili adhabu kali zichukuliwe dhidi yao.
Maadhimisho ya siku ya mwanamke anayeishi kijijini, yalianza kuadhimishwa rasmi mwaka 2007 chini ya Azimio la Umoja wa Mataifa, ikiwa na lengo kuimarisha ustawi wa maendeleo ya mwanamke kijijini kwa kuhakikisha mwanamke anapata mahitaji yake muhimu ikiwemo maji safi, lishe bora, afya ya uzazi, nishati bora pamoja na kumlinda dhidi ya vitendo vya ukatili.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.