Na. Elinipa Lupembe.
Shirika la SOS Kjijiji cha Watoto Tanzania, limekabidhi zahanati yake, kwa halmashauri ya Arusha, lengo likiwa kuendelea kushirikiana na serikali, kuboresha upatikanaji rahisi wa huduma za afya kwa wananchi wa eneo la Mji mdogo Ngaramtoni.
Akizungumza wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya zahanati hiyo iliyopewa jina la Kishore, iliyofanyika kwenye Kijiji cha watoto SOS Ngaramtoni, Mwenyekiti wa Bodi wa shirika la SOS Tanzani, Haruna Masebo, ameweka wazi kuwa shirika hilo, limeamua kukabidhi zahanati hiyo kwa serikali, lengo likiwa ni kuongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya kwa wananchi, sambamba na kuunga mkono juhudi za serikali za kupunguza vifo vya kina mama na watoto wakati wa kujifungua.
Mkurugenzi wa Shirika la SOS, David Mulongo, amesema kuwa shirika la SOS, lililianzishwa kwa lengo la kusaidia watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu pamoja na kuendesha miradi ya elimu na afya, kwa sasa shirika limeamaua kujikita kwenye malengo yake ya awali, katika kutoa huduma kwa watoto pekee na kuwapa wadau wengine ikiwemo serikali kuendeleza miradi ya elimu na afya ambayo ilisimamiwa na shirika.
Ameongeza kuwa, SOS kwa kukabidhi zahanati hiyo ya Kishore kwa serikali ni kusogeza karibu huduma za afya kwa wananchi wa eneo la Ngaramtoni, kufuatia mikakati ya serikali ya kuwa na zahanati katika kila kijiji.
Hata hivyo mkurugenzii huyo wa SOS, ameipongeza serikali kwa jitihada za kuboresha huduma za jamii kwa kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na zahanati na kila kata ina kituo cha afya, kutokana na uhitaji wa zahanati katika eneo hilo, kumesababisha shirika kukabidhi kwa serikali, ili huduma itolewe kwa watu wote.
Naye mkurugezni mtendaji, halmashauri ya Arusha, Selemani Msumi licha ya kulishukuru shirika hilo la SOS, amewapongeza kwa kushirikiana na halmashauri hiyo, kutoa huduma za kijamii kwa maendeleo ya ustawi wa jamii ya watanzania na kuongeza kuwa serikali inathamini sana michango ya wadau hasa katika sekta ya maendeleo ya jamii na kuahidi kusimamia kituo hicho kutoa huduma bora na endelevu kwa kipindi chote.
Awali mkurugezni Msumi, amezitaja baadhi ya huduma muhimu ambazo zimekuwa zikitolewa na shirika la SOS kwa halmashauri ya Arusha, ni pamoja na kulea watoto yatima na wale wanaoishi kwenye mazingira magumu, kusaidia ukarabati wa miundombinu ya shule, kutoa mikopo kwa vikundi vya wajasiriamali pamoja na kuzijengea uwezo kamati za kupinga ukatili dhidi ya wananwake na watoto MTAKUWWA ngazi ya kata.
"Ninafahamu namna SOS mmetusaidia katika mambo mengi kwenye sekta ya elimu na afya, lakini msichoke kutusaidia, niombe mtupatie gari la wagonjwa, kwa kuwa halmashauri yetu ina eneo kubwa na kuna uhitaji mkubwa wa gari la kubebea wagonjwa, ambalo litasaidia kunusuru vifo vya wagonjwa ambao wanatakiwa kufanyiwa rufaa kwenda kupata matibabu kwenye hospitali za wilaya, mkoa na zile za rufaa" amesisitiza Mkurugenzi Msumi.
Hata hivyo wakazi wa eneo la Ngaramtoni na vitongoji vyake, wamelishukuru shirika la SOS kwa kuwapatia Zahanati ambayo itawawezesha kupata huduma za afya kwa karibu, huku wakiitaka halmashauri yao kuleta wahudumu wa afya wenye weledi katika kuhudumia wananchi pamoja na dawa za kutosha kwa kuwa tayari zahanati hiyo ina vifaa vya kutosha.
Diwani wa kata ya Olturumet, mheshimiwa Joseph Tinayo, amesema kuwa, zahanati hiyo imekuja wakati sahihi, kwa kuwa wanachi wa eneo hilo walikuwa na uhitaji wa huduma za afya kutokana na umbali uliopo kutoka eneo hilo mapaka kufika hospitali ya wilaya ya Olturumet.
Naye Liliani Mungaya aliyefika zahanati hapo kwa mara ya kwanza na kupata chanjo ya UVIKO 19, amebainisha kuwa, ingawa zahanati hiyo ilikuwa hapo, lakini wananchi wengi hawakuwa huru kufika hapo, kupata matibabu wakidhani kuwa zahanati hiyo ilikiwa kwa ajili ya Kijiji cha Watoto wa SOS tu.
"Tunaishukuru SOS na halmashauri kwa kukubaliana na kukabidhiana zahanati hii, kwa kuwa kwa sasa wananchi wa Ngaramtoni tutakuwa huru kuja kutibiwa hapa, kupitia bima zetu za Jamii, hapa ni karibu na zahanati ina vifaa vya kutosha, ni jukumu la serikali sasa, kutuletea madaktari na wauguzi wakutosha watakaotutibu" amesema Liliani,
Kijiji cha watoto SOS Arusha kilianzishwa rasmi mwaka 1991, na shirika la SOS wakiwa na lengo la kuhudumia watoto yatima, watoto wanaokaribia kupoteza familia na wanaoishi kwenye mazingira magumu kwa kuanzisha makazi ya watoto ndani ya kijiji, huku shirika likifanikiwa kuhudumia takribani watoto 600.
Mwenyekiti wa Bodi SOS Tanzania Haruni Masebo (wa kwanza kushoto) Haruna Masebo na Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Selema Msumi, wakikata utepe, kama ishara ya makabidhiano ya zahanati ya Kishore iliyokuwa inamilikiwa na SOS.
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi (katikati) akionesha hati ya mkataba wa makabidhiano wa Zahanati ya Kishore mara baada ya kusainiwa baina ya uongozi wa halmashauri ya Arusha na shirika la SOS.
Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, akitia saini mkataba wa makabidhiano wa Zahanati ya Kishore baina ya uongozi wa halmashauri ya Arusha na shirika la SOS.
Mwenyekiti wa Bodi wa shirika la SOS Tanzani, Haruna Masebo, akitia saini mkataba wa makabidhiano wa Zahanati ya Kishore kati ya shirika hilo na halmashauri ya Arusha.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.