Halmashauri ya Arusha kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la SNV, wametoa mafunzo kwa vijana kutoka kata 11 halmashauri hiyo, juu ya udodosaji na ukusanyaji wa takwimu za hali za vyoo kwenye maeneo yao kwa njia ya mtandao.
Mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uwezo vijana wa kukusanya takwimu ili kufanya tathmini ya hali halisi ya vyoo kwenye kata ambazo zimeonekana kutokufanya vizuri kwa kaya kuwa na vyoo bora.
Mshauri wa Masuala ya Usafi wa Mazingira shirika la SNV, Anna Emmanuel na mwezeshaji wa mafunzo hayo, amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo vijana wa kudodosa na kukusanya takwimu za hali za vyoo katika maeneo yao kwa njia ya mtandao.
Ameongeza kuwa, matarajio ya ukusanyaji wa takwimu hizo ni kupata takwimu zitakazowezesha kufahamu, hali halisi ya vyoo kwenye kaya pamoja na kufanya tathmini ya hali za vyoo endapo kuna athari yoyote ya vyoo iliyotoka na mvua zinazoendelea kunyesha.
Mmoja wa vijana waliohudhuria mafunzo hayo, Robert Aloyce wa kijiji cha Mbuyuni kata ya Oljoro amesema kuwa, kwa sasa wananchi wameanza kuelewa umuhimu wa kuwa na vyoo bora licha ya kuwa bado wanakabiliwa na changamoto ya uelewa mdogo wa juu ya unawaji mikono.
Ameongeza kuwa bado jamii inahitaji elimu zaidi juu ya unawanaji wa mikono kwa kuwa watu wengi hawajui wakati hasa na namna bora ya unawaji mikono.
" Wananchi wamehamasika kujenga vyoo, lakini sio watu wengi wanafahamu namna bora ya unawaji mikono, watu wengi hawafahamu wakati hasa wa kunawa mikono" amesema Aloyce .
Afisa Afya halmashauri ya Arusha, Issa Msumari amesema kuwa, licha ya wananchi kujenga vyoo bora lakini bado kunahitajika uhamasishaji wa unawaji mikono, ambao unachangia kwa asilimia kubwa maambukizi ya magonjwa yanayotokana na kinyesi.
Hata hivyo Msumari ameitaka jamii kuzingatia suala zima la unawaji mikono na kufafanua nyakati muhimu wa kunawa mikono ni mara baada ya kutoka chooni, kabla ya kuandaa chakula, kabla ya kula na kabla ya kunyonyesha mtoto kwa kina mama wanaonyonyesha.
Kata zitakazokusanywa takwimu hizo ni pamoja na kata ya Oldonyowas, Oldonyosambu, Olkokola, Lemanyata, Musa,Kisongo, Oljoro, Bwawani, Nduruma,Olturoto na Ilkiding'a.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.