Na. Elinipa Lupembe.
Vijana katika Halmashauri ya Arusha, Wilaya ya Arumeru, wametakiwa kuhudhuria kwenye Vituo Vya Afya, kupata mafunzo Afya ya uzazi na Uzazi wa mpango kupitia Huduma Rafiki kwa Vijana, huduma inayotolewa kupitia Mradi wa Tupange pamoja, mradi unaotekelezwa na halmshauri, kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la JHPIEGO.
Rai hiyo imetolewa na Mratibu wa Shirika la JHPIEGO Mkoa wa Arusha, Waziri Njau, katika semina ya mafunzo ya Afya ya Uzazi kwa vijana kupitia Huduma Rafiki kwa Vijana, mafunzo yaliyofanyika kwenye Ofisi ya Kata ya Moivo, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Njau amesema, kwa kawaida, elimu ya Afya ya Uzazi na Uzazi wa mpango, hubadilika kutokana na tafiti mbalimbali zinaendelea kufanywa na wanasayansi, hivyo ni vyema kuhudhuria mafunzo hayo, mara kwa mara ili kufahamu zaidi juu ya afya ya Uzazi na uzazi salama.
"Elimu ya Afya ya Uzazi, iliyotolewa zamani ni tofauti na elimu ya sasa kutokana, maendeleo ya sayansi na teknolojia, yamesababisha kugundulika kwa dawa na vimelea mbalimbali ambavyo hapo awali havijulikani" amesema Njau
Naye Mratibu wa Tupange pamoja kata ya Moivo, Kylie Gyubi, amesema vijana wanapaswa kujitambua na kutambua afya zao, kwa kutembelea vituo vya Afya na kukutana na wataalamu wa afya ya uzazi salama ili kupima na kupata ushauri juu ya Afya ya uzazi.
"Vijana wengi wamekuwa wakitumia njia za uzazi wa mpango bila kufuata ushauri wa wataalam wa afya, jambo linawasababisha kupata madhara kiafya na kudhani kuwa njia hizo sio salama, kumbe tatizo ni taarifa zisizo sahihi juu ya dawa hizo" amesema Gyubi
Hata hivyo vijana hao wamekiri kuwa na taarifa zaidi za Uzazi wa Mpango kuliko afya ya Uzazi, kutokana na ukweli kwamba mara nyingi, huduma hiyo hutolewa kwa vijana ambao tayari wamepata watoto na kuanza kuhudhuria kliniki.
Wamethibitisha kufuta ujinga nje ya shule, kutokana na elimu waliyoipata iliyowawezesha kufahamu kuwa, afya ya uzazi ni zaidi ya uzazi wa mpango, inayomuwezesha kijana kutambua mabadiliko ya mwili wake, jinsi ya kuishi na kuyamudu mabadiliko hayo, kujikinga na mimba za utotoni, mimba zisizotarajiwa bila kutumia dawa zisizo rasmi, kujiandaa kwa ajili ya kuanzisha familia pamoja na kujikinga na magonjwa yanayotokana na ngono zembe hasa gonjwa hatari la UKIMWI.
Kijana Juma Saidi, amesema kuwa kutokana na ukosefu wa taarifa sahihi za afya ya uzazi kwa vijana, vijana wengi wamejikuta wakiingia kwenye mgogoro wa malezi ya watoto bila kujipanga, huku wasichana wakikatiza masomo kwa ajili ya mimba, kutokana na uelewa mdogo juu ya afya ya uzazi kwa vijana.
"Vijana wengi wamejikuta wanalazimika kuoana kwa kuwa tayari wameshapeana mimba, na kuanza majukumu ambayo hawakuwa wamejipanga jambo ambalo, linasababisha ndoa hizo kuvunjika na kuingia kwenye migogoro mikubwa na kuwa na ongezeko kubwa la watoto wa mitaani" amesema kijana huyo.
Aidha Said ameongeza kuwa, vijana wengi hufundishana wenyewe na kuanza kujamiiana, huku wengi wakuamini kuwa, ukimuandaa msichana vizuri, na kujamiiana ndani ya dakika tano, hawezi kupata maambukizi ya UKIMWI, taarifa ambayo si za kweli, tendo la kujamiiana linaweza kuambukiza magonjwa ya ngono, kansa ya shingo ya kizazi na ugonjwa wa UKIMWI.
Naye Raja Matela licha ya kuishukuru timu ya Tupange Pamoja kwa kuwapatia elimu hiyo, ameiomba timu hiyo kuendelea kutoa elimu hii kwa jamii, ili kubadili mtazamo hasi na kuwafanya kuwa mabalozi wazuri katika kuhamasisha Afya ya uzazi na Uzazi wa mpango na Huduma Rafiki kwa Vijana,. kwani itasaidia kupunguza vifo vya mama na mtoto na kuwa na uzazi salama.
"Kabla ya kupata elimu hii tulikuwa tunafahamu kuwa unapotumia njia za uzazi wa mpango kwa mwanamke huharibu umbile lake lakini kasasa tumegundua si kweli kwamba njia za uzazi wa mpango haziwezi kuharibu umbile la mwanamke" amesema kijana huyo
Afisa Vijana, halmashauri ya Arusha, Ahadi Mlai, amewataka vijana hao, kukutana kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi, ili kujifunza na kuongeza maarifa juu ya Afya ya uzazi na Uzazi wa mpango, na kuongeza kuwa kwa sasa 'Huduma Rafiki kwa Vijana', imeanza kutolewa kwenye vituo 15 vya kutolea huduma za Afya, ndani ya hamashauri hiyo na kuwasisitiza vijana, kufika kwenye vituo hivyo kupata taarifa sahihi juu ya Afya ya Vijana.
Mradi wa Tuwavushe salama hutoa fursa kwa vijana kujiongezea maarifa, uelewa, ujuzi na mbinu juu ya Afya uzazi na Uzazi wa mpango kwa kutumia njia salama zitakazo punguza vifo vya mama na mtoto.
Vijana wa kata ya Moivo, wakisikiliza mafunzo ya elimu ya Afya ya Uzazi kwa vijana, kwenye ofisi ya kata ya Moivo.
Mratibu wa Tupange pamoja kata ya Moivo, Kylie Gyubi, akifundisha vijana njia ya asili ya uzazi wa mpango kwa kutumia zana halisi.
Mratibu wa Shirika la JHPIEGO Mkoa wa Arusha, Waziri Njau, akitoa mada kwa vijana, juu ya Afya ya Uzazi na Uzazi wa mpango kwa vijana.
Vijana wakiendelea na mafunzo
Afisa Vijana, halmadhauri ya Arusha, Ahadi Mlai, akitoa mada wakati wa mafunzo ya Afya ya Uzazu na uzazi wa mpango kwa vijana.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.