Na Elinipa Lupembe
Vijana halmasahuri ya Arusha, wameshauriwa kuachana na migogoro ya ardhi wanazozirithi kutoka kwa baba na babu zao, badala yake kutafuta maeneo yao binafsi, nje ya mkoa huo kwa kuwa Tanzania bado ni kubwa na ina maeneo mengi ambayo bado hayajatumika.
Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti, halmashauri ya Arusha, Mhe. Ojung'u Salekwa, wakati akifunga Kampeni ya Msaada wa Kisheria bure, iliyofanyika kwenye viwanja vya KKKT kata ya Ilkiding'a, halmashauri ya Arusha na kufafanua kuwa migogoro ya ardhi imekuwa ni tishio kwenye familia nyingi na jamii kwa ujumla.
Amesema kuwa wananchi wengi wa halmashauri hiyo wamejikuta wanakabiliwa na migogoro ya ardhi, inayotokana na mila na desturi za kurithishana ardhi kutoka kizazi hadi kizazi, huku idadi ya watu ikiongezeka wakati ardhi haiongezeki tangu enzi na enzi.
Mwenyekiti Ojung'u, amewashauri wananchi hao hususani vijana ambao bado wana nguvu, kutafuta ardhi kwenye maeneo mengine ya Tanzania badala ya kuendelea kung'ang'ania, ardhi za mababu zinazowasababishia migogoro, uadui na umaskini kwa kutumia pesa nyingi kuendesha kesi.
"Ni kweli thamani ya ardhi Arusha iko juu lakini niwasihi vijana, wenye nguvu, kwa kuwa Tanzania bado ina maeneo mengi, tafuteni ardhi zenu kwenye maeneo mengine nchini, badala ya kuendelea kung'ang'ania ardhi za urithi, maeneo ambayo kimsingi ni madogo hayatoshelezi kulinganisha na idadi ya watu kwa sasa". Amesisitiza Mwenyekiti Ojung'u.
Endapo vijana wataamua kuachana na ardhi za urithi na kutafuta kumiliki ardhi kwenye maeneo mengine mbali na maeneo ya familia, itakuwa ni njia moja wapo ya kuondokana na migogoro kwa njia mbadala kama watalamu wa sheria walivyoshauri, njia ambayo itaondoa uhasama, uadui lakini zaidi itaondoa umasikini wa kupambana na kesi, kesi ambazo wengi wametumia pesa nyingi mpaka kufilisika.
Naye Diwani wa kata ya Sambasha, Mhe. Francis Lukumay, licha ya kuishukuru serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kwa kuwapa fursa wananchi kupata msaada wa kisheria bure, amebainisha kuwa bado wananchi wanahitaji elimu zaidi juu ya usuluhishi wa mogogoro kwa njia mbadala.
"Wananchi wamejifunza mambo mengi ya kisheria, mambo ambayo hapo awali wengi wetu hatukuyafahamu, tumefahamishwa utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala, hivyo tuendelee kuwatumia watalamu wetu wanatoa msaada wa kiaheria bure kupata utatuzi wa migogoro katika jamii yetu". Amebainisha mhe. Diwani Lukumay
Kaimu Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria, Laurent Burilo, ameweka wazi kuwa Kampeni iliyofanyika imeonyesha mafanikio makubwa sana, kwa kutoa mwelekeo wa kuwa kuna uhitaji mkubwa wa msaada wa kisheria kwa wananchi, hivyo kuna umuhimu wa wasaidizi wa kisheria kuwasaidia wananchi kutatua migogoro yao kwa njia mbadala.
Aidha amezitaja huduma zilizotolewa wakati wa Kampeni hiyo ni pamoja na kutoa elimu ya utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala, haki za watoto, ukatili dhidi ya wanawake na watoto pamoja na kutoa msaada wa kisheria bure kwa watu wasio na uwezo juu ya migogoro ya ardhi na mipaka, urithi na mirathi, pamoja na migogoro ya ndoa na familia.
Kampeni ya Kutoa msaada wa kisheria kwa wananchi bure, yenye kauli mbiu ya "Utatuzi wa Migogoro kwa njia Mbadala, hupunguza Uadui na kuziua umaskini", imefanyika kwa siku tatu katika kata ya Ilkiding'a, ikijumuisha wakazi wa kata hiyo na kata za jirani za Sambasha, Olturoto na Kiranyi.
ARUSHA DC TUPO KAZINI
KAZI INAENDELEA✍✍
Mwenyekiti halmashauri ya Arusha, Mhe. Ojung'u Salekwa, akizungumza wakati wa kufunga Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a
Kaimu Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria, Laurent Burilo, akisoma tathmini ya Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a.
Diwani wa kata ya Ilkiding'a Mhe. Francis Lukumay, akizungumza na wananchi waliofika kwenye Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a.
Mwenyekiti wa Jumuia ya Wazazi CCM kata ya Ilkiding'a Paulo Ngarabali akitoa ushuhuda wa namna jumuia hiyo inapambana na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto katika kata yake wakati wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a.
Mwezeshaji wa TASAF Halmashauri ya Arusha, Kabula Sukwa, akitoa mada ya Haki na Wajibu wa wanakaya walio kwenye Mapngo wa Kunususru kaya Masikini, wakati wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a.
Baadhi ya wananchi wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa Kampeni ya Msaada wa Kisheria, iliyoandaliwa na Wizarara ya Katiba na Sheria na kufanyika kwenye viwanja vya kanisa la KKKT Ilkiding'a.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.