Na Elinipa Lupembe.
Wakufunzi wa Sensa ya Watu na Makazi mkoa wa Arusha, wametakiwa kuwa waadilifu, wazalendo na kutumia weledi wa hali ya juu katika kufanikisha zoezi la Sensa, inayotarajiwa kufanyika nchini tarehe 23, August 2022.
Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongela, wakati akifunga mafunzo ya siku 21 kwa wakufunzi wa Sensa ngazi ya mkoa, mafunzo yaliyofanyika, kwenye ukumbi wa mikutano chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) .
Mkuu huyo wa mkoa amewataka wakufunzi hao, ambao watakwenda kuwafundisha makarani wa maudhui ya Sensa ngazi ya Halmashauri, kwenda kufanya kazi hiyo kwa uadilifu, uzalendo na weledi hasa kwa kuzingatia umuhimu na madhumuni ya Sensa ya Watu na Makazi kwa wananchi na serikali kwa ujumla.
"Kwa kutambua umuhimu wa Sensa ya watu na makazi, serikali imewaamini na kuwapa mafunzo ya muda mrefu ili muweze kufanyakazi hiyo kwa weledi kwa kuzingatia kanuni na taratibu za kazi hiyo, hivyo ni vema mkatambua mnakwenda kufanya kazi nyeti kwa manufaa ya Taifa letu la Tanzania" Amesisitiza Mkuu huyo wa mkoa.
Hata hivyo Mhe. Mongela, amesisitiza kuwa endapo mtakwenda kuwafundisha makarani wa Sensa kwa weledi, mtaiwezesha serikali kupanga mipango yake ya maendeleo kwa kuzingatia idadi ya watu ambao zoezi la kufanikisha hili liko mikononi mwenu, niwatake mkafanye kazi hii kwa kujiamini kama serikali ilivyowaamini.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi mkoa wa Arusha, Steven Zelote, amewasihi wakufunzi hao, kufanya kazi hiyo vema na kuhakikisha mkoa wa Arusha unakuwa kinara wa Sensa ya Watu na Makazi nchini.
Naye mwanasemina na Afisa Elimu kata ya Olmotonyi, halmashauri ya Arusha, mwalimu Denis Machallo, amesema kuwa, wanatambua umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi kwa serikali yao, hivyo kupitia mafunzo hayo, wameahidi kwenda kufanya kazi hiyo kwa weledi hasa kwa kuzingatia mustakabali wa Taifa la Tanzania na kwa kuweka uzalendo mbele na kuhakikisha wanahawilisha maarifa waliyoyapata kwa makarani wa maudui ngazi za halmashauri kama ilivyo malengo ya serikali.
"Tumepewa mafunzo kwa siku 21, wawezeshaji wamefanya kazi yao vema, hivyo tunakwenda kutekeleza jukumu hili la kitaifa, kwa kuzingatia maslahi mapana ya taifa letu la Tanzania na sio vinginevyo ili kuhakikisha zoezi la Sensa linafanikiwa kwa zaidi ya asilimia 100 katika mkoa wetu wa Arusha". Amesisitiza Mwalimu Machallo.
Awali mkufunzi mkuu wa mafunzo hayo, Mdoka Omari, ameweka wazi kuwa, jumla ya wakufunzi 399 kutoka halmashauri zote 7 za mkoa wa Arusha, wamepatiwa mafunzo ya Sensa ya Watu na Makazi ambao watakwenda kuwafundisha makarani wa sensa katika halmashauri zao.
*SENSA YA WATU NA MAKAZI 2022*
*JIANDAE KUHESABIWA*✍
Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongela, wakati akifunga mafunzo ya wakufunzi wa Sensa ya Watu na Makazi ngazi ya Mkoa, mafunzo yaliyofanyika, kwenye ukumbi wa mikutano chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) .
Wakufunzi wa Sensa ya watu na Makazi ngazi ya Mkoa wa Arusha, wakimskiliza mkuu wa mkoa wa Arusha, mhe. John Mongela wakati akifunga mafunzo hayo, kwenye ukumbi wa mikutano chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) .
Mkufunzi mkuu wa mafunzo mkoa wa Arusha, Mdoka Omari akisoma taarifa ya hali halisi ya mafunzo hayo wakati wa kuhitimisha mafuzo hayo, yaliyofanyika, kwenye ukumbi wa mikutano chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) .
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, mkoa wa Arusha Steven Zelothe (wa kwanza kulia) akiwa kwenye hafla ya kufunga mafunzo kwa wakufunzi wa Sensa ngazi ya mkoa, kwenye ukumbi wa mikutano chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) .
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.