Na Elinipa Lupembe.
Kufuatia mkakati wa Serikali wa kufikia Ajenda 10/30 ya Kilimo Biashara, halmashauri ya Arusha, inaendelea tekeleza mpango huo kwa vitendo kwa kuwapati vikundi vya wakulima wanaojishughulisha na kilimo cha mbogamboga kata ya Sambasha, mafunzo ya kilimo bora cha kisasa na chenye tija.
Akizunguza na mwandishi wa habari hizi, Afisa Kilimo kata ya Sambasha Anna Lorry, amethibitisha kuwa jumla ya wakulima 155 wa kata hiyo, wamepatiwa mafunzo kupitia shamba darasa lililopo eneo la Tengeru, lengo likiwa ni kuwajengea uwezo wa kufanya kilimo cha kisasa, kitakachowawezesha kufanya biashara kupitia mazao wanayolima.
Afisa Kilimo huyo amebainisha kuwa, kwa sasa wakulima wa eneo hilo wameanza kubadilika na kulima kisasa kwa kutumia eneo dogo na kuzalisha mazao mengi, na kuachana na kilimo cha mazoea, ambacho kiliwapatia faida ndogo.
"Wakulima wamefundishwa kutumia eneo dogo kupata mazao mengi, uchaguzi wa mbegu bora, matumizi ya mbolea na dawa sahihi za kuulia wadudu pamoja na kufanya tafiti za masoko kabla ya kuamua kulima zao husika kulingana na msimu" . Amefafanua Afisa Kilimo huyo.
Hata hivyo wakulima hao licha ya kuishukuru Serikali kwa kuwa na mikakati imara kwao, wamekiri mafunzo hayo kuwapa ujuzi na maarifa mapya ikiwa ni pamoja na mbinu sahihi za kuwawezesha kufanya kilimo biashara, jambo ambalo wamekiri hapo awali waliliona kama ni ndoto.
Wameongeza kuwa, mafunzo hayo yamewatoa kwenye kilimo cha cha mazoea na kuwaaminisha kwamba kilimo biashara kinawezekana kupitia maeneo yao, wanayoyatumia kulima kwa miaka yote, ambayo walitumia nguvu na gharama kubwa na kupata faida kidogo.
"Awali sikuelewa Kilimo biashara nilidhani ni propaganda tuu, kupitia mafunzo mbalimbali tunayopatiwa na serikali kwa kushirikiana na wadau wa kilimo, ninatumia ujuzi nilioupata, ninaamini kilimo biashara inawezekana na tunaweza kufikia Ajenda 10/30 kwa vitendo" . Amesema Mosses Njivai mkulima kijiji cha Shibolo.
Njivai amethibitisha kuwa, awali hatukuwa tunafanya tafiti za masoko kabla ya kulima, jambo ambalo lilisababisha kuuza mazao kwa bei ya hasara kutokana na mafuriko ya mazao wakati wa mavuno, program ya Anzia Sokoni Malizia Shambani kwa kipato zaidi inatufanya kuwa watafiti wa masoko kabla ya kulima.
Awali Halmashauri ya Arusha kwa kushirikiana na wadau wa kilimo, wanaendelea kutoa elimu na mbinu za kilimo bora kwa wakulima, lengo likiwa ni kuongeza pato la mkulima na kufikia Agenda 10/30 ya Kilimo Biashara.
ARUSHA DC TUPO KAZINI
AJENDA 10/30 TUNATEKELZA
KAZI INAENDELEA ...✍✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.