Na Elinipa Lupembe ARUSHA DC
Wananchi halmashauri ya Arusha hususani wakuu wa kaya, wametakiwa kutoa ushirikiano kwa makarani wa Sensa, wakati wote wa zoezi la Sensa ya watu na makazi kwa kutoa taarifa zote sahihi zinazohitajika kwenye dodoso la Sensa.
Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa wilaya ya Arumeru, wakati wa kuhitimisha Matembezi ya Hiari ya kuhamasisha Sensa ya watu na makazi, kwenye stendi ya Ngaramtoni, Katibu Tawala wa wilaya hiyo, Mwl. James Nchembe, amewataka wananchi wa halmashauri hiyo hususani wakuu wa kaya, kutoa ushirikiano kwa makarani wa Sensa watakapofika kwenye kaya zao kukusanya taarifa za Sensa.
Amesema kuwa kwa kufanya hivyo, kutawezesha makarani hao kupata taarifa sahihi zitakazowesha kupata takwimu sahihi zinazohitajika na Serikali kwa ajili ya kupanga mipango yake sahihi kwa maendeleo ya watanzania wote..
"Utoaji na upatikanaji wa Takwimu sahihi utawezesha serikali na wadau wengine kupanga mipango ya maendeleo ya watu wake katika sekta ya elimu, afya, hali ya ajira, miundombinu ya barabara, maji safi na nishati, mipango ambayo itawezesha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi". Amesistiza Katibu Tawala huyo.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, ameeleza kuwa lengo la matembezi hayo ya hiari ni kuhamasisha wanachi wa halmashauri hiyo, kushiriki zoezi la Sensa ya watu na makazi na kuhakikisha kila mtu amehesabiwa siku hiyo ya tarehe 23.08.2022 na kuwasisitiza wakuu wa kaya kuhakikisha kila mtu aliyelala kwenye kaya yake siku hiyo amehesabiwa.
Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, Mhe. Noah Lembris, ameeleza kuwa suala la Sensa ya watu na makazi ni jambo la muhimu sana kwa wananchi wa Jimbo hilo, na kuwasihi wananchi wote kuhakikisha wamehesabiwa ili serikali iweze kuoanga mipango ya maendeleo katika jimbo hilo.
Monica Lema mkazi wa Oloirien, amewataka wananchi wote kuhakikisha wamehesabiwa siku hiyo ya Sensa ya Watu na makazi, jambo litakalosadia kuweza kupata maendeleo kwani serikali itajua idadi sahihi ya Watu ambayo itawezesha serikali kupata takwimu sahihi kwa ajili ya kupanga kwa usahihi utoaji wa huduma za msingi kutokana na takwimu za idadi ya watu.
Katika matembezi hayo, halmashauri kwa kushirikiana na wadau wa afya, wameweza kutoa huduma za kupima afya bure kwa wananchi wote walifika kwenye shughuli hiyo katika eneo la Ngaramtoni ikiwemo ugonjwa, homa ya ini, saratani ya shingo ya kizazi, UKIMWI, kisukari na shinikizo la damu.
HAKIKISHA UMEHESABIWA 23.08.2022
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.