Na. Elinipa Lupembe.
Jumla ya walimu 22 wa mchezo wa soka kwa shule za msingi, wamepata mafunzo ya siku tano, yaliyofanyika katika shule ya msingi Ngaramtoni, halmashauri ya Arusha.
Mafunzo hayo yametolewa kwa lengo la kuwajengea walimu hao uwezo wa kufundisha wanafunzi soka taaluma, linaloendana na maendeleo ya Sayansi na teknolojia.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa shirika la Future Star Accademy, Kocha Mkufunzi, Alfredd Itaeli amesema kuwa, kupitia mafunzo hayo mwalimu wamejengewa uwezo wa kuwafundisha watoto mbinu za kisasa za kucheza soka zinazoendana na umri wao na kwa kuzingatia zaidi wakati uliopo.
Amesema kuwa, mwalimu amefundishwa kutoka kwenye mbinu za zamani za kufundisha soka na kujifunza mbinu za kisasa, ikiwa ni pamoja na kumfanya mwalimu kuwa na mbinu zinazoendana na wakati.
"Tunawatoa walimu kwenye soka la kuwafanyisha watoto mazoezi magumu, ya kupanda na kushuka milima, ya kuruka kichura mazoezi yanayoharibu misuli, badala yake wachezaji kufanya mazoezi yanayojenga mwili na kuimarisha misuli na mchezaji kuwa imara.
Afisa Utamaduni, halmashauri ya Arusha, Priscus Steven amewataka walimu kwenda kutumia taaluma waliyoipata, kuwafundisha wanafunzi na si kuifunika taaluma hiyo kwa kuicha kwenye makaratasi.
Aidha amewataka walimu kuvaa uhusika wa kufundisha michezo hasa wawapo uwanjani kwani haiba ya mwalimu huwajenga watoto zaidi.
"Walimu vaeni uhusika wakati wa kufundisha soka, unapokuwa uwanjani vaa mavazi ya michezo, unakuta mwalimu anawafundisha watoto amevaa jeans, hii haikubaliki na inapunguza morari ya michezo kwa watoto" amesema Afisa huyo.
Hata hivyo walimu hao wamekiri kujifunza mbinu mpya za ufundishaji wa soka, mbinu zinazoendana na umri wa watoto, aina ya mazoezi ya kujenga pamoja na muda sahihi wa kufanya mazoezi.
Mwalimu wa soka, shule ya Msingi Olmotony, mwalimu Aziza Laizer, amesema kuwa, mafunzo hayo yamewatoa kwenye mbinu za kizamani walizokuwa wanatumia kufundisha watoto na kuwajengea mbinu za kisasa ambazo wanaamini zitasaidia kuwajenga wanafunzi kwenye soka taaluma.
Kadhalika, mwalimu wa michezo, shule ya msingi Loovilukuny, Severine Rock, amekiri walimu wengi wa michezo kufundisha kwa uzoefu bila mafunzo yoyote huku wakitumia mbinu za kizamani, mbinu ambazo haziendani na umri wa wanafunzi na muda.
"Walimu wengi wa michezo wanatumia uzoefu tuu, kufundisha soka lakini kupitia mafunzo hayo nimejifunza mbinu mpya na nimeweza kutambua kuwa nilikuwa nawafundisha watoto soka bila kuzingatia muda wala umri wa watoto" amesema mwalimu Rock.
Mafunzo hayo yamedhaminiwa na shirika la Ace Africa kwa kushirikiana na Future Star Accademy mashirika yanayosimamia mchezo wa soka kwenye shule 11 ndani ya Tarafa ya Mukulat, halmashauri ya Arusha.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.