Na. Elinipa Lupembe.
Wazazi wa wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka wa masomo 2022, shule ya sekondari Einoti kata ya Kisongo, wameamua kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita, inayoongozwa na Mhe. Rais Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kujenga choo cha wavulana chenye matundu 7 shuleni hapo.
Wazazi hao wamefikia hatua hiyo ya kuchanga fedha za kujenga vyoo vya wavulana shuleni hapo, baada ya serikali kutoa fedha, kiasi cha shilingi milioni 120 za kujenga vyumba 6 vya madarasa, viti na meza 300, kupitia fedha za mapambano dhidi ya UVIKO 19, mwishoni mwa mwaka uliopita wa 2021, madarasa ambayo, yamekamilisha upungufu wa vyumba vya madarasa shuleni hapo.
Akizungumza wakati wa kukabidhi, matundu hayo ya vyoo kwa mkurugenzi mtendaji halmashauri ya Arusha, Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi na Mwenyekiti wa Kijiji cha Engorora Mhe. Justine Leiyan, amesema baada ya watoto wao kuchaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza shule ya sekondari Einoth na kukuta serikali imejenga madarasa 6, kwa ajili ya wanafunzi hao wa kidato cha kwanza mwaka 2022, walikaa na kuamua kujenga matundu ya vyoo vya wanafunzi wa kiume.
"Kama wazazi tuliona serikali imejenga madarasa 6 kwa ajli ya watoto wetu, na sisi tuchangie nguvu kwa kuchanga elfu 30 kwa kila mzazi na kupata shilingi milioni 6.3, za kujenga choo cha wavulana, tukiwa na lengo la kuwahakikishia watoto wetu, wanasoma kwenye mazingira bora kwa ulinzi wa afya zao wawapo shuleni" ameweka wazi Mwenyekiti Justine.
Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, licha ya kuwashukuru wazazi hao kwa kuunga mkono juhudi za serikali, amewapongeza kwa juhudi za kuhakikisha watoto wao wanasoma katika mazingira yanayowahakikishia afya bora shuleni pamoja na kuwafanya kuboreka kwa maendeleo yao kitaaluma.
"Ninathamini, ninashukuru na ninawapongeza sana kwa namna ya kipekee wazazi wote, miliojitoa na kuhakikisha watoto wenu wanapata sehemu ya kujistiri, jambo ambalo linaporesha mazingira ya kuhakikisha afya bora ya watoto wawapo shuleni, niwahakikishie serikali inatambua na kuthamini mchango wenu, kwa maendleo ya Taifa letu" amefafanua Mkurugenzi Msumi
Aidha amewataka wazazi hao kuwasimamia na kuwasaidia watoto wao kukamilisha ndoto zao kwa kuwapa mahitaji yatakayowawezesha kusoma kwa bidii na kuhakikisha wanafikia elimu ya juu, ili waweze kupata maarifa na kuwa watalamu, watakaowezesha maendelo ya Taifa la Tanzania.
"Usimdhulumu mtoto wako kwa kumkatisha masomo, jitahidi kuwekeza kwenye elimu, mpe mtoto wako fursa ya kupata elimu, ili apate maarifa na utalamu, ukimkatisha mtoto masomo, utakuwa kwanza umedhulumu kwa kumkatisha ndoto zake, tusiwe sehemu ya dhuluma ya kukosesha taifa letu watalamu katika sekta mbalimbali hapo baadaye". Amesisitiza Msumi
Hata hivyo Diwani wa kata ya Kisongo, Mheshimiwa Godson Loningo, amesema kuwa wananchi wa Kisongo, wanatambua juhudi zinazofanywa na serikali ya awamu ya sita, ya kuborehsa miundo mbinu shuleni hapo, na kuongeza kuwa wameguswa na kuona umuhimu wa kuchangia maendeleo ya shule kwa manufaa ya watoto wao.
"Tunatambua juhudi za serikali pamoja na juhudi za walimu wa shule hii ya kuwafundisha watoto, shule ina maendeleo na mafanikio kimiundombinu na kitaaluma, kupitia mafanikio hayo, wazazi wajitoa kwa hali na mali kuhakikisha shule hii inakua na kusimama kama shule nyingine kongwe" amefafanua Mheshimiwa Diwani
Victoria Samke, mmoja wa wazazi mwenye mtoto wa kidato cha kwanza, amewahamasisha wazazi wenzake kupambana kwa ajili ya watoto na kuhakikisha wanapata elimu bora ndani ya eneo yao, jambo ambalo hapo zamani halikiwepo, watoto walifuata elimu mbali na kuwafanya wazazi wengine kushindwa kuwasomesha watoto.
Mkuu wa shule sekondari Einoth mwalimu Justine Swai, licha ya kuwapongeza wazazi kwa kazi kubwa na ya thamani, waliyoifanya kwa shule hiyo, zaidi amewashukuru wazazi hao kwa kuwalea na kuwasimamia watoto wao vizuri, kwa kuwa ni watoto wenye maendeleo mazuri kitaaluma, nusu ya wanafunzi wamepata daraja la I kwenye mitihani ya robo ya kwanza ya mwaka 2022.
Shule ya sekondari Einoth iliyoka kata ya Kisongo, ni miongoni mwa shule za kata zinazokua kwa kasi kiataaluma na kimiundo mbinu, ilioanza mwaka 1996, mpaka sasa ina jumla ya wanafunzi 989 wasichana 595 na wavulana 390.
ARUSHA DC
KaziInaendelea✍
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.