Na. Elinipa Lupembe.
Wazazi wenye watoto wanosoma shule za kutwa halmashauri ya Arusha, wamekumbushwa jukumu lao la kuchangia chakula cha watoto wao wawapo shuleni, kufuatia Sera ya Elimu bila malipo ya mwaka 2015 16, hivyo wasikwepe majukumu yao, kwa kivuli cha serikali kutoa elimu bila malipo.
Rai hiyo imetolewa na mkurugenzi mtendaji halmashauri ya Arusha, Selemani Msumi, alipokuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya kuwaaga wanafunzi wa kidato cha nne mwaka 2021, shule ya sekondari Sokon II, mahafali yaliyofanyika kwenye viwanja vya shule hiyo.
Mkurugenzi Msumi ameyasema hayo, mara baada ya mkuu wa shule hiyo mwalimu Prisca Mbele, kuwasilisha changamoto zinazoikabili shule hiyo, ikiwemo wazazi kutokuchangia chakula cha watoto wao, jambo ambalo linaathiri sana tendo la kujifunza kwa wanafunzi, na kukwamisha kiwango cha taaluma shuleni hapo, kutokana wanafunzi wengi kushinda na njaa kutwa nzima, wawapo shuleni.
Amewataka wazazi kutambua kuwa Sera ya Serikali ya kutoa elimu bila malipo, inabainisha wazi kiwa ni jukumu la mzazi kuchangia chakula cha mchana kwa wanafunzi wanaosoma shule za kutwa, na kuwasisitiza wazazi kuwa na huruma na watoto wao, kwa kuwa tendo la kujifunza linahitaji kutumia akili nyingi, na ukiwa na njaa kimsingi akili haifanyi kazi kwa ufanisi.
"Ili mtoto aweze kufaulu vizuri anahitaji kuwa na afya bora, afya bora inatokana na kupata lishe bora, lishe inayoyokana na chakula, wazazi kuweni na huruma, huo ni ukatili, hata tujenge madarasa, tuwe na walimu wakutosha, walimu wafundishe kwa juhudi zote, kama mwanafunzi ana njaa ni kazi bure, wazazi liangalieni hilo kwa jicho la imani" amesisitiza Mkurugenzi huyo.
Aidha Mkurugenzi Msumi, amewapongeza wananfunzi hao wa kidato cha nne kwa hatua waliyofikia na kuwasihi kujiandaa vema na mitihani yao ya Taifa, kwa kusoma kwa bidii ili waweze kufaulu vizuri huku akiwasisitiza kwamba, kuhitimu kidato cha nne ndio mwanzo wa safari ya mafaniko yao, hivyo wanatakiwa kuwa waadilifu na wenye nidhamu ya hali ya juu, pindi wawapo nyumbani wakisubiri matokeo yao ya mtihani wa Taifa.
"Someni kwa kwa bidii, someni kwa malengo, huku mkitambua kuwa uwezo wa kufanya vizuri mnao, tambueni kuwa nyinyi ni wathamani, na mnategemewa na Taifa hili, huko duniani mnakokwenda epukeni vishawishi, wasichana wangu 'is not too late to say no' msidanganyike na vishawishi, msikubali kuuza utu wenu kwa chipsi, wala msikubali kujiingiza kwenye mahusiano ya kimapenzi katika umri mdogo" amesisitiza Mkurugenzi Msumi
Hata hivyo mkurugenzi Msumi ameahidi kutoa kiasi cha shilingi laki 5 kwa ajili ya kuchangia ununuzi wa mashine ya kudurufu karatasi shuleni hapo, pamoja na kuongoza harambee ya kupata fedha za kununua vitabu vya kiada na ziada katika shule hiyo, ambapo jumla ya shilingi 1,198,000 zilipatikana huku fedha taslimu zikiwa ni shilingi 708,000 na ahadi shilingi 490,000.
Nao wanafunzi wanaohitimu kidato cha nne, 2021, wameushukuru uongozi wa shule hiyo, walimu wao, wazazi na walezi kwa malezi bora waliyowapatia kipindi chote cha miaka minne, walipokuwa shuleni hapo, na kuwaahidi kufanya vizuri katika mtihani wao wa Taifa, kwa kuwa tayari wameandaliwa vema na wanaamini watafaulu kwa viwango vya juu.
Aidha wahitimu hao wa kidato cha nne, wameiomba Serikali kuendela kutatua changamoto zinazoikabili shule hiyo, ikiwemo ukosefu wa maji shuleni hapo, ufinyu wa eneo la shule, upungufu wa vitabu vya ziada na kiada pamoja kuwataka wazazi kugharamia chakula cha watoto wao wawapo shule kwani wanafunzi wengi hushinda njaa shuleni, jambo ambalo hukwamisha zoezi zima la kujifunza kwao na kuwafanya wanafunzi kuishi kwa mateso wawapo shuleni.
Awali, shule ya sekondari Sokoni II ni moja kati ya shule za kata inayokua kwa kasi kubwa, iliyoanzishwa kwa jitihada za wananchi wa eneo hilo mwaka 2015, ikiwa na wanafunzi 50, mpaka sasa ina jumla ya wanafunzi 1,092, huku wanafunzi 206 wakihitimu kidato cha nne mwaka 2021, wasichana 120 na wavulana 87, ikiwa ni mahafali ya tano tangu kuanzishwa kwa shule hiyo.
ARUSHA DC
KaziInaendelea ✍✍✍✍✍
PICHA ZA MATUKIO KATIKA MAHAFALI YA 5 SEKONDARI SOKON II
Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi akikagua miundo mbinu ya shule ya sekondari Sokoni II muda mfupi kabla ya kuanza sherehe za mahafali ya kidato cha nne, 2021 shuleni hapo.
Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi akizungumza na hadhara ya Jumuia ya wanaSokon II, walimu, wanafunzi na wazazi na wageni waalikwa wakati wa sherehe za mahafali ya kidato cha nne, 2021 Sekondari ya Sokoni II.
Mkuu wa shule ya Sekondari Sokon II Mwl. Prisca Mbele, akisoma risala ya shule hiyo, mbele ya mgeni rasmi wakati wa mahafali ya kidato cha nne, 2021, yaliyofanyika kwenye viwanja vya shule hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi akimkabidhi cheti Gift Elisante Abednego, mwanafunzi bora kwa wahitimu wa kidato cha nne 2021, wakati sherehe za mahafali shuleni hapo.
Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi akimkabidhi cheti Laurine Simoni Swai, mwanafunzi bora, aliyeongoza kimasomo kwa wasichana wa kidato cha nne, wakati sherehe za mahafali ya kidato cha nne, 2021 shuleni hapo.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.