Jumla ya wazee 61 wa kata ya Kiutu kati ya wazee 692 wa halmashauri ya Arusha wamepata uhakika wa matibabu baada ya kukabidhiwa kadi za matibabu za Mfuko wa Afya ya Jamii 'CHF', zoezi liliofanyika kwenye ofisi ya kata ya Kiutu.
Wazee hao wamekabidhiwa kadi za Bima ya Afya zitakazowawezesha kutibiwa bure kwenye vituo vyote, vinavyotoa huduma za afya ndani ya halmashauri ya Arusha.
Akizungumza wakati wa kukabidhi kadi hizo, Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha Dkt. Wilson Mahera amesema halmashauri imefika hatua hiyo, mara baada ya kugundua adha wanayoipata wazee ya kugharamia matibabu pindi wanapougua.
Wazee ambao kwa kiasi kikubwa kwa namna moja au nyingine walilitumikia taifa hili la Tanzania pindi wakiwa na nguvu zao na serikali imeona ni vema kuwathamini na kuendelea kuwatunza ili kuenzi michango yao ya kuijenga nchi hii.
Aidha Dkt. Mahera amesema kuwa kuwapa wazee kadi za bima ya afya ni mkakati wa serikali ya awamu ya tano, wa kuhakikisha wazee wanakuwa na uhakika wa kupata matibabu pindi wanapougua.
"Serikali imepanga mikakati thabiti ya kuboresha miundombinu ya vituo vyake vya kutolea huduma za afya, pamoja na kuhakikisha uwepo wa vifaa tiba na dawa ili kurahisishia watanzania upatikanaji wa matibabu muhimu kwenye maeneo yao" amesema Mkurugenzi Mahera.
Naye Diwani wa kata ya Kiutu, Mhe. Zephania Sirikwa amemshukuru mkurugenzi na uongozi wa halmashauri ya Arusha, kutenga fedha kwa ajili ya kuwahudumia wazee hasa katika matibabu na kuongeza kuwa licha ya wazee hao kuwa na uhakika wa matibabu lakini pia kadi hizo zitawapunguzia makali ya gharama za matibabu pindi watakapougua.
Hata hivyo Kaimu Mganga Mkuu, halmashauri ya Arusha Dkt. Peter Mboye amethibitisha uwepo wa madirisha maalumu ya kuwahudumia wazee kwenye vituo vya afya na hospitali ya wilaya.
Maadirisha ambayo ni maalumu kwa lengo la kuwapunguzia adha wazee adha ya kukaa muda mrefu wafikapo kupata huduma ya afya.
Dkt. Mboye amewahakikishia wazee hao uwepo na upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vya kutolea huduma kutokana na serikali kuboresha sekta ya afya.
Mratibu wa Bima ya Afya ya Jamii halmashauri ya Arusha, Agrey Ngoka amesema kuwa, jumla ya wazee 692 watapewa vitambulisho hivyo, vitakavyotolewa kwa wazee wa kata 14 kwa awamu ya kwanza, vitambulisho vilivyogharimu shilingi milioni 8.7.
Hata hivyo Ngoka amefafanua kuwa leo wamezindua kwa kutoa vitambulisho kwa wazee 61 wa kata ya Kiutu na zoezi la ugawaji vitambulisho hivyo litaendelea kwenye kata 13 zilizobaki.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.